Polisi waonya Gen Z maadhimisho ya maandamano ya Juni 25 yakikaribia
POLISI wameidhinisha kwa masharti maandamano ya vijana wa Gen Z yanayopangwa kufanyika Juni 25 kote nchini, wakisema waandalizi wana uhuru wa kufanya maandamano ya amani lakini wakaonya kwamba hawataruhusu uvunjaji wa sheria au kuvurugwa kwa shughuli za kawaida.
Haya yanajiri huku waandalizi wa maandamano wakihimiza Wakenya kutotoka nyumbani siku hiyo.
Maandamano hayo yanapangwa kuadhimisha mwaka mmoja tangu kuuawa kwa makumi ya vijana wakati wa maandamano ya kupinga Mswada wa Fedha wa mwaka 2024.
Ingawa waandalizi wamewahimiza Wakenya kubaki majumbani siku hiyo na kutaka biashara pamoja na shule kufungwa, maafisa wa usalama wameeleza wasiwasi kuhusu mwito huo wakihofia unaweza kutumiwa na wahuni kuzua fujo.
Afisa mmoja wa cheo cha juu wa polisi alisema vikosi vya usalama vimepewa maagizo ya kuchukua hatua za haraka dhidi ya dalili zozote za vurugu.
“Tutawaruhusu kufanya maandamano yao kama inavyotakiwa katika Katiba, lakini tutakuwa macho kuhakikisha hakuna uvunjaji wa sheria,” alisema afisa huyo.
Polisi pia wanahofia uwezekano wa maandamano hayo kuvamiwa na wahuni, jambo ambalo limewahi kushuhudiwa katika maandamano ya awali na kusababisha uharibifu wa mali na mapigano.
Duru zinasema kuwa Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja aliongoza mkutano wa ngazi ya juu wa makamanda wa polisi katika Chuo cha Uongozi wa Polisi cha Ngong ili kupanga mikakati ya kukabiliana na vitendo vya wahuni wakati wa maandamano hayo.
Katika notisi iliyowasilishwa kwa Huduma ya Kitaifa ya Polisi, waandalizi walisema wataandaa maandamano ya amani kuelekea Bunge la Kenya ili kudai haki kwa waliouawa wakati wa maandamano ya mwaka jana na kuweka maua katika maeneo walikopotezea maisha.
Pia kutakuwa na mikusanyiko na shughuli za kumbukumbu katika kaunti zote 47 nchini.
Familia za waliouawa wakati wa maandamano ya Juni 2024 ziliwasilisha notisi hiyo kwa polisi Alhamisi, zikiambatana na viongozi mbalimbali akiwemo aliyekuwa Jaji Mkuu Willy Mutunga, kiongozi wa PLP Martha Karua, Gavana wa Siaya James Orengo, wakili Gitobu Imanyara na mkurugenzi wa Muslims for Human Rights, Khelef Khalifa.
Mama yake Rex Masai, mmoja wa vijana waliouawa wakati wa maandamano hayo, alisema familia hizo zinataka maafisa wote waliohusika na mauaji, mateso na kutoweka kwa watu wafikishwe mahakamani.
Pia wanataka Juni 25 itangazwe kuwa siku ya kitaifa ya kumbukumbu na kujengwa kwa mnara wa kuwakumbuka vijana waliopoteza maisha.
Kwa mujibu wa Tume ya Kitaifa ya Haki za Kibinadamu (KNCHR), watu wasiopungua 50 waliuawa kati ya Juni 18 na Julai 16 mwaka 2024 wakati wa maandamano ya kupinga Mswada wa Fedha.
Maandamano hayo yalifikia kilele Juni 25, 2024 wakati waandamanaji walipovamia majengo ya Bunge baada ya wabunge kupitisha mswada huo uliozua utata.
Kutokana na shinikizo kubwa za umma, serikali baadaye iliondoa mswada huo huku Rais William Ruto akivunja Baraza lake la Mawaziri kabla ya kuunda serikali jumuishi iliyowahusisha baadhi ya viongozi wa upinzani.
Viongozi walioandamana na familia hizo wamewataka polisi kuheshimu Katiba na kuhakikisha hakuna umwagikaji damu wakati wa maadhimisho hayo.
Bw Mutunga alisema vijana wa Gen Z wamefufua ari ya kutetea Katiba na haki za wananchi.
Kwa upande wake, Gavana Orengo alisema ni muhimu siku za Juni 25 na 26 zitambuliwe kama siku za kukumbuka waliouawa na kujeruhiwa.
Naye Profesa Kivutha Kibwana aliwataka polisi kujizuia kutumia nguvu kupita kiasi.
“Damu ya vijana isije ikamwagika tena Juni 25,” alisema.
Waandalizi sasa wanasubiri polisi kutekeleza ahadi yao ya kutoa usalama wakati wa maandamano hayo ya kumbukumbu yanayotarajiwa kuvutia maelfu ya Wakenya kote nchini.