Nyoro alazimika kujitetea baada ya kuhepa kura ya Mswada wa Fedha
MBUNGE wa Kiharu, Ndindi Nyoro, amelazimika kujitetea baada ya kukosolewa vikali kwa kutokuwa bungeni wabunge walipopigia kura Mswada wa Fedha wa 2026. Mswada huo ulipitishwa na Bunge la Kitaifa kwa kura 122 dhidi ya 40, na sasa unasubiri kutiwa saini na Rais William Ruto ili kuwa sheria.
Hata hivyo, ni wabunge 162 pekee kati ya 349 waliohudhuria kikao hicho muhimu, hali iliyozua maswali kuhusu ushiriki wa wabunge katika maamuzi muhimu ya taifa.
Nyoro, ambaye amekuwa mmoja wa wakosoaji wakuu wa baadhi ya mapendekezo ya ushuru yaliyomo kwenye mswada huo, alilaumiwa vikali na wananchi waliotarajia angekuwepo kupiga kura.
Akizungumza kupitia mtandao wa X Ijumaa, mbunge huyo alisema hakuwa nchini wakati kura ilipopigwa kutokana na shughuli za kikazi ambazo hangeweza kuahirisha.
“Kura ya Mswada wa Fedha ilifanyika jana. Kwa masikitiko makubwa sikuwa bungeni. Nilisafiri nje ya nchi Jumatano jioni kwa shughuli ambazo hazingeweza kuahirishwa. Hakuna maelezo yanayoweza kuondoa lawama hizo,” alisema.
Nyoro aliongeza kuwa amepokea maoni ya Wakenya kwa unyenyekevu na kusisitiza kuwa maoni ya wananchi ni muhimu katika kuimarisha uwajibikaji wa viongozi na usimamizi wa uchumi.
Mbunge huyo pia alitetea rekodi yake ya kushiriki mijadala ya masuala ya fedha bungeni, akisema amekuwa mstari wa mbele kutoa maoni mbadala kuhusu Mswada wa Fedha na Mswada wa Matumizi ya Serikali.
Aidha, Nyoro alidai kuwa uwezo wa Bunge kusimamia serikali umeathirika kutokana na viongozi wa pande zote mbili za Bunge kuwa na misimamo inayofanana katika masuala mengi.
Pia alieleza kuwa pendekezo lake la kupunguza bei ya mafuta halikujumuishwa katika ripoti ya Kamati ya Fedha. Alisema juhudi zake za kuwasilisha pendekezo hilo kupitia mswada wa kibinafsi zilikwama.