Familia yalilia msaada kurejesha mwili wa jamaa aliyefariki DRC
FAMILIA moja katika mji wa Kitale, Kaunti ya Trans Nzoia, inaendelea kupitia majonzi makubwa baada ya kushindwa kurejesha nyumbani mwili wa jamaa yao aliyefariki katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) wiki tatu zilizopita kutokana na vikwazo vya usafiri vinavyohusishwa na mlipuko wa Ebola.
Familia ya marehemu Wycliffee Makheti Muchaka, ambaye alikuwa fundi mitambo katika eneo la Durba kaskazini mashariki mwa DRC, sasa inaomba serikali kuingilia kati ili kusaidia kuurejesha mwili wake nchini kwa mazishi.
Muchaka alienda DRC kutafuta ajira na alikuwa akifanya kazi huko kwa kibali cha muda kwa takriban mwaka mmoja na nusu. Kulingana na jamaa zake, alikuwa akiwasiliana mara kwa mara na familia yake hadi walipopokea taarifa za kushtua kuhusu kifo chake mnamo Mei 30, 2026.
Familia ilielezwa na jirani kuwa marehemu alipatikana akiwa amekufa katika mazingira yasiyoeleweka kando ya barabara karibu na makazi yake mjini Durba.
Mwili wake kwa sasa umehifadhiwa katika Hospitali ya Centre Hospital Kibali, lakini familia inasema imepewa onyo kwamba huenda ukazikwa huko ikiwa hautachukuliwa haraka.
Mama yake, Bi Hellen Muchaka, alisema familia imekuwa katika maumivu makubwa kwa siku 22 tangu kifo hicho kutokea huku juhudi za kuurejesha mwili zikikwama.
“Tumehesabu siku 22 tangu afariki lakini bado hatujafaulu kumleta nyumbani. Gharama za kuhifadhi mwili zinaendelea kuongezeka na tumefadhaika sana,” alisema kwa huzuni.
Jamaa mwingine, Benjamin Wamalwa, alisema watu wawili wa familia pamoja na madereva wa gari la kubeba maiti walielekea mpaka wa Uganda na DRC mnamo Juni 12 kwa lengo la kuchukua mwili huo lakini walizuiwa kuingia DRC kutokana na masharti yaliyowekwa kufuatia mlipuko wa Ebola.
“Walirudishwa bila mwili. Taarifa tulizopewa ni kwamba hakuna aliyeruhusiwa kuingia DRC kutokana na hali ya Ebola,” alisema.
Familia inasema bili ya kuhifadhi mwili imeendelea kuongezeka na sasa wanahitaji zaidi ya Sh300,000 ili mwili utolewe.
Kutokana na changamoto hizo, wameomba Wizara ya Masuala ya Kigeni na Wakenya wanaoishi ng’ambo kusaidia kusafirisha mwili huo kwa ndege hadi Kenya.
“Tunaomba serikali na viongozi wetu watusaidie ili tumzike ndugu yetu kwa heshima. Utamaduni wetu haukubali wapendwa wetu kuzikwa ugenini,” alisema Bi Muchaka.
Familia hiyo sasa ina matumaini kuwa serikali itaingilia kati na kusaidia kuurejesha mwili wa mpendwa wao nyumbani kwa mazishi ya heshima.