Mataifa 7 ya Afrika yatinga hatua ya 32 Bora Kombe la Dunia 2026
MATAIFA saba kati ya 10 yanayoiwakilisha Afrika katika Kombe la Dunia la mwaka huu, tayari yamefuzu kwa hatua ya mwondoano ya timu 32 bora.
Ghana na Cape Verde ndiyo timu za hivi karibuni kuhakikisha nafasi zao kufuatia matokeo ya mechi za Jumamosi usiku.
Ghana ilifuzu licha ya kuwa bado ina mechi moja ya mwisho ya kundi dhidi ya Croatia. Kufuzu kwa Black Stars kulithibitishwa baada ya Uhispania kuichapa Uruguay 1-0, matokeo yaliyowafanya Waghana washindwe kuondolewa kwenye nafasi za kufuzu.
Cape Verde nayo ilikata tiketi baada ya kutoka sare kwa mara ya tatu mfululizo kwenye mashindano hayo. Matokeo hayo yaliifanya imalize nafasi ya pili katika kundi lao nyuma ya Uhispania.
Timu hizo mbili zimeungana na Misri, Morocco, Afrika Kusini, Senegal na Ivory Coast ambazo tayari zimehakikisha nafasi katika hatua ya mwondoano.
Hata hivyo, safari ya Tunisia imefikia tamati baada ya kuondolewa kwenye mashindano hayo.
Kwa upande mwingine kufikia Jumamosi, Algeria na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo zilikujwa hazijafuzu lakini, bado zilikuwa na matumaini ya kusonga mbele ikiwa tu rekodi zao zitatosha kuwafanya kuwa miongoni mwa timu bora zilizomaliza nafasi ya tatu katika makundi.
Katika mfumo mpya wa Kombe la Dunia uliopanuliwa kutoka timu 32 hadi 48, timu mbili bora kutoka kila moja ya makundi 12 zitafuzu moja kwa moja hatua ya 32 bora. Aidha, timu nane bora zilizomaliza nafasi ya tatu pia zitapata tiketi ya kuendelea.
Baada ya hatua ya 32 bora, mashindano yataendelea kwa hatua ya 16 bora, robo fainali, nusu fainali, mechi ya kusaka mshindi wa nafasi ya tatu na hatimaye fainali itakayochezwa Julai 19.
Kwa mara ya kwanza katika historia ya Kombe la Dunia, FIFA imetumia rekodi ya matokeo ya timu zilizofungana (head-to-head) kama kigezo cha kwanza cha kuvunja sare badala ya tofauti ya mabao.
Kwa mujibu wa kanuni za mashindano hayo, iwapo timu mbili au zaidi zitamaliza hatua ya makundi zikiwa na idadi sawa ya pointi, nafasi zao zitaamuliwa kwa kufuata vigezo vilivyowekwa na FIFA, vikianza na matokeo ya mechi walizocheza kabla ya kuangalia vigezo vingine vya ushindani.