2027: Mudavadi kimya watu wakijipanga
KIMYA na kukosekana kwa Kinara wa Mawaziri Musalia Mudavad katika mjadala wa nani atakuwa mgombeaji mwenza wa Rais William Ruto mnamo 2027 kumeibua maswali kuhusu mikakati yake ya kisiasa.
Miezi michache iliyopita, kumekuwa na wito kutoka kwa viongozi mbalimbali kuhusu wale ambao wanastahili kuwa mgombeaji mwenza wa Rais Ruto 2027.
Ndani ya Serikali Jumuishi, wanasiasa kutoka Mlima Kenya wamekuwa wakishinikiza wadhifa wa mgombeaji mwenza usalie kwa Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki.
Baadhi ya viongozi wa Magharibi mwa Nchi nao wanampigia upato Spika wa Bunge la Kitaifa, Moses Wetangula kwa wadhifa huo.
Ndani ya ODM kuna kambi mbili ambazo zimezuka ambapo baadhi ya wanasiasa kutoka Pwani wanampigia upato Waziri wa Madini, Hassan Joho.
Kwa upande mwingine wanasiasa kutoka Magharibi mwa Nchi nao wanamtaka Waziri wa Vyama vya Ushirika, Wycliffe Oparanya.
Ndani ya upinzani, Kiongozi wa Linda Mwananchi, Edwin Sifuna ambaye anatoka Magharibi kama tu Bw Mudavadi, ameshabikiwa awe mgombeaji mwenza au hata mwaniaji wa urais.
Mjadala kuhusu mgombeaji mwenza wa Rais Ruto ukishika, hakuna mwanasiasa anayeonekana kumakinikia Bw Mudavadi na haijulikani iwapo bado anataka kuwa rais baada ya uchaguzi mkuu wa 2027.
Waziri huyo wa Masuala ya Kigeni amekuwa akimakinikia ziara ya Rais nje ya nchi akionekana kutomakinikia siasa za nchi.
Mnamo Juni 13, akiwa ameandamana na Rais Ruto katika hafla ya kisiasa katika Chuo Kikuu cha Masinde Muliro, aliwaonya wakazi wa Magharibi dhidi ya kuingia mtego wa upinzani.
“Kuna watu ambao wanajifanya wanatoa mwelekeo kwa jamii yetu ilhali walibanduliwa madarakani na hawajui hatima yao. Kama viongozi wenu tumeamua kuunga mkono kuchaguliwa tena kwa Rais Ruto,,” akasema Bw Mudavadi.
“Nilikuambia mnamo 2022 kuwa yeye ndiye njia na sasa bado ndiye njia. Lazima tusalie tumemakinika na watu wetu wasidanganywe,” akongeza Bw Mudavadi.
Waziri huyo, Bw Wetangúla na Bw Oparanya wanachukuliwa kama viongozi wakongwe kutoka Magharibi ambao wametawala siasa za eneo hilo kwa miaka mingi.
“Shida ya Wetangúla na Mudavadi ni kwamba wanafikiria umri wao hausongi na ule wa Rais Ruto unasonga. Wetangula atakuwa na miaka 75 mnamo 2032 naye Mudavadi 71. Mbona wahisi watapewa urais na tunastahili kuwasubiri? Kama wangekuwa makini wao ndio wangekuwa wakimpa Rais Ruto mamlaka,” akasema Bw Natembeya.
Seneta wa Kakamega, Boni Khalwale naye anasema wakati huu watu wa Magharibi hawako na Bw Mudavadi na Wetangúla.
“Sitaki nizungumze nionekane nawadharau ila ukweli ni kwamba mara hii watu hawako nao,” akasema Seneta huyo.
Seneta wa zamani wa Kakamega, Cleophas Malala ambaye ni naibu kiongozi wa DCP pamoja na wabunge Raphael Wanjala (Budalangí) na Junnet Mohamed (Suna Mashariki) pia wanampigia upato Bw Oparanya.
Kwa upande mwingine Gavana wa Kakamega, Fernandes Baraza naye amemtaja Bw Wetangúla kama kigogo wa siasa wanayemuunga mkono kurithi nafasi ya Rais Ruto na hata anatosha kuwa mgombeaji mwenza.
“Amekuwa nje ya nchi kwa mikutano na Rais Ruto na nahisi anaweza kuteuliwa mgombeaji mwenza wake. Wetangúla anaonekana kifua mbele kuliko Mudavadi kwa sababu amekuwa nyanjani na bado ana chama chake cha Ford Kenya,” akasema Profesa Masibo Lumala, msomi na mchanganuzi wa masuala ya kisiasa.