Wakenya waliotimuliwa Afrika Kusini wazungumzia masaibu yao
BAADHI ya Wakenya wamesimulia kwa uchungu jinsi ambavyo walilazimika kurejea nchini kutoka Afrika Kusini ambako wenyeji wanawafurusha wageni.
Juni 30 ilikuwa makataa ambayo raia wa Afrika Kusini walitoa kwa wahamiaji haramu kuondoka nchini humo wakiwakashifu kwa kunyakua nafasi za ajira pamoja na kutumia rasilimali zao.
Ingawa Wakenya hawajalengwa sana, wiki jana serikali ilianza kuwarejesha nchini wale ambao wanatilia shaka usalama wao.
Anthony Waweru ambaye amekuwa Afrika Kusini tangu 2022 akiwa dereva wa basi alisimulia jinsi ambavyo nyumba yake ilichomwa. Alisema alisikia kundi la watu likikaribia kwake usiku likiimba kwamba raia wa kigeni lazima waondoke bila mali yoyote.
“Nilitoka mahala hapo wiki mbili zilizopita na kuenda kwingine kujificha,” akasema.
Bw Waweru alikuwa kati ya Wakenya 55 ambao walitua uwanja wa JKIA Alhamisi iliyopita saa 11 asubuhi. Alinufaikia mpango wa serikali wa kuwarejesha Wakenya wanaoishi nchini humo ambao usalama wao upo hatarini.
Kufikia Jumamosi, serikali ilikuwa imewarejesha Wakenya 266 nchini kupitia mpango huo ambao Wizara ya Masuala ya Kigeni imesema utafikia tamati mnamo Alhamisi hii.
“Wakenya ambao wanataka kurejeshwa nchini wanastahili kujisajili na ubalozi wa Kenya Afrika Kusini jijini Pretoria kufikia Alhamisi,” ikasema wizara hiyo kupitia taarifa mnamo Ijumaa jioni.
Bi Ruth Wambui, mfanyabiashara naye alirejea na watoto wake wawili akisema alikuwa kati ya wale ambao walitishiwa na hakuwa na budi ila kurejea nchini.
“Mwanzoni nilikuwa sijaamua kurudi lakini baada ya kuona hasara na mali ambayo nimepoteza, nimeona ni afadhali nirejee nchini,” akasema.
Alifichua kuwa nyumba yake iliteketezwa mwaka jana katika njia tatanishi na pia biashara yake ilikuwa ikilengwa.