Habari Mseto

Matonya: Waliniseti kuhusu kesi ya ubakaji Kenya

Na SINDA MATIKO July 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MWANAMUZIKI mkongwe wa bongo flava Matonya ameamua kurejea nyumbani Tanzania baada ya mahakama ya Mombasa kumfutia makosa ya ubakaji.

Matonya alikuwa akiishi Mombasa kabla ya kukumbwa na kesi hiyo na kupelekewa kukamatwa kwake Aprili mwaka huu na kusotea jela kwa zaidi ya wiki mbili kabla ya kuachiliwa kwa bondi.

Akizungumza na safu hii baada ya kurejea kwao Tanzania, Matonya alidai kuwa kesi hiyo ilikuwa ya kutengenezwa na ndio sababu aliishia kuachiwa na mahakama ya Shanzu kule mombasa, baada ya ushahidi kukosekana.

”Mahakama za Kenya sasa zimenipa uhuru rasmi na kwenda kuendelea na shughuli zangu. kikweli nina mengi ya kusema kuhusu haswa kilichotokea lakini wanasema ukiwa na furaha sana au ukiwa na hasira sana, unatakiwa uchunge ulimi yako. Kwa hiyo furaha niliyonayo inaweza ikazidi ikanifanya niongee yasiyofaa ila niseme Alhamdhulilah,” Matonya alitanguliza kusema.

Kuhusu haswa kwa nini aliweza kufutia madai, Matonya alisisitiza kuwa ni kutokana na kuwa kesi ile ilikosa mashiko.

“Sijui kesi hiyo limetokeatokeaje, lilitengenezwatengenezwaje mpaka likanikuta nilipokuwa, ila nimewasamehe. Ila pamoja na yote kwa ndugu zangu Wakenya siko tayari kupoteza upendo tulioutengeneza ndani ya miaka 19 kwa tatizo la watu wachache.”

Matonya alikamatwa baada ya kudaiwa kumbaka mmoja wa rafiki zake, maeneo ya kule Nyali, Mombasa mapema mwezi Aprili.