Habari za Kitaifa

Kenya yageuzwa ngome ya wahuni sasa wakitumiwa kutwaa ardhi, biashara na mali

Na PETER MBURU July 22nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KENYA inaendelea kugeuka kuwa paradiso ya wahuni wanaotumiwa kutwaa ardhi, nyumba, biashara na mali nyingine huku amri za mahakama zikipuuzwa na mamlaka zikionekana kushindwa kuwalinda waathiriwa.

Katika miaka ya hivi karibuni, makundi ya vijana wenye silaha yamekuwa yakihusishwa na uvamizi wa hospitali, kufurusha familia kutoka nyumba zao, kutwaa majengo ya biashara na kuzuia utekelezaji wa amri halali za mahakama.

Mojawapo ya visa vinavyoibua wasiwasi ni kile cha Hospitali ya Nakuru War Memorial, ambayo imefungwa kwa zaidi ya miaka miwili licha ya mahakama kuagiza ifunguliwe tena.

Msimamizi mkuu wa wauguzi wa hospitali hiyo, Patricia Musale, anasema mgogoro ulianza Oktoba 2023 alipopigiwa simu akiarifiwa kuwa kundi la watu lilikuwa limevamia hospitali likidai limechukua usimamizi wake.

Alipofika, lango kuu lilikuwa limefungwa na akalazimika kuruka ua kuingia ndani.

“Muda mfupi baadaye, maafisa wa kaunti walichukua udhibiti wa hospitali na wagonjwa wote wakaanza kuhamishwa. Kabla ya usiku wa manane, kila mgonjwa alikuwa ameondolewa, wakiwemo watoto waliokuwa kwenye mashine za kuwasaidia kupumua,” alisema.

Hospitali ilipata amri za mahakama za kufunguliwa tena lakini kabla ya kutekelezwa, kundi jingine la zaidi ya vijana 200 lilivamia eneo hilo Januari 2024 na kuzuia mtu yeyote kuingia.

“Tulipata amri kadhaa za mahakama lakini kila tunapofika tunawakuta wahuni wamezingira lango. Hata polisi wakifuatana nasi hakuna kinachofanyika,” alisema Bi Musale.

Kwa zaidi ya miaka miwili sasa, vifaa vya matibabu vya thamani ya mamilioni ya pesa vimekaa bila kutumika huku wafanyakazi wengi wakipoteza ajira na wagonjwa waliokuwa wakitegemea huduma kama za figo na matibabu ya Virusi vya Ukimwi wakiteseka.

Mzozo huo unatokana na mgogoro wa umiliki wa ardhi kati ya hospitali na Serikali ya Kaunti ya Nakuru.

Mnamo Februari 2024, Jaji Mkuu Martha Koome alieleza wasiwasi kuhusu uvamizi huo na ukaidi wa amri za mahakama, lakini hadi leo hospitali haijafunguliwa.

Kisa kingine kinachoonyesha jinsi wahuni wanavyotumiwa kutwaa mali ni cha mfanyabiashara Avan Shah wa Nairobi.

Bi Shah anasema Novemba 2022 dalali aliwasili nyumbani kwake akiwa ameandamana na takriban watu 30 waliokuwa na mapanga na marungu.

“Walidai wanatekeleza amri ya mahakama. Kabla hatujathibitisha stakabadhi walikuwa tayari wameanza kubomoa nyumba. Polisi walifika lakini hawakutusaidia,” alisema.

Familia hiyo ilifurushwa kutoka nyumba waliyoishi kwa karibu miaka 50 na hadi sasa haijarejea huku kesi ikiendelea mahakamani.

Kamati ya Ardhi ya Bunge la Kaunti ya Nairobi baadaye ilibaini kuwa kulikuwa na dosari katika usimamizi wa rekodi za ardhi hiyo na kupendekeza hatua zichukuliwe dhidi ya maafisa waliohusika.

Visa hivi vinaonyesha mwenendo unaozidi kushika kasi ambapo migogoro ya ardhi, biashara na mali haiamuliwi tena mahakamani pekee bali pia kwa nguvu za makundi ya wahuni.

Katika maeneo mengi nchini, wahuni hutumiwa kuwafurusha wapangaji, kufunga njia za kuingia katika majengo yanayobishaniwa, kutwaa biashara na hata kuzuia utekelezaji wa amri za mahakama.

Hata madalali wanasema mara nyingi hulazimika kufanya kazi katika mazingira ya vitisho na ghasia.

Wakenya wengi wanaishi kwa hofu kwamba siku moja wanaweza kupokonywa nyumba, biashara au ardhi yao kwa nguvu licha ya kuwa na haki kisheria.

Kwa wengi, hali hiyo inaashiria hatari kubwa kwa utawala wa sheria, ambapo nguvu za makundi ya wahuni zinaanza kushinda mamlaka ya mahakama katika kuamua nani anamiliki mali nchini.