Serikali yakubali ukosoaji wa ufadhili elimu ya juu; yaweka mpango wa ‘kufaidi wote’
WANAFUNZI wote watakaofuzu kujiunga na vyuo vikuu nchini watapata ufadhili kamili wa masomo kutoka kwa serikali iwapo pendekezo jipya la ufadhili wa elimu ya juu litapitishwa na Bunge.
Rais William Ruto alitangaza hatua hiyo Jumanne katika Ikulu, akisema serikali imewasilisha mapendekezo ya marekebisho ya sheria yatakayowezesha kila mwanafunzi anayefaulu mtihani wa kitaifa na kupata nafasi katika chuo kikuu au taasisi ya elimu ya juu kufadhiliwa kikamilifu bila kujali hali ya kifedha ya wazazi wake.
“Kwa sasa tuna pendekezo bungeni litakalowezesha elimu ya juu kuwa ya wote. Haitajali mtoto anatoka katika familia gani, bali uwezo wake kitaaluma. Mwanafunzi yeyote anayefaulu na kupata nafasi chuoni atapata ufadhili kamili,” alisema Rais Ruto.
Aliwahimiza wabunge kuharakisha kupitisha marekebisho ya sheria ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HELB) ili wanafunzi watakaoanza masomo Septemba mwaka huu wanufaike kwa mfumo huo mpya.
Tangazo hilo linaashiria kuwa serikali inaweza kuachana na mfumo wa sasa wa ufadhili wa elimu ya juu ulioanzishwa mwaka wa 2023 ambao umekoselewa na wanafunzi, wazazi na wadau wa elimu.
Rais alisema mfumo wa awali haukufaulu kwani ulisababisha vyuo vikuu vingi kukumbwa na matatizo ya kifedha baada ya serikali kushindwa kutoa kiwango cha fedha ilichoahidi.
“Baadaye tukaanzisha mfumo wa usawa ambapo wazazi walichangia sehemu ya karo, serikali ikatoa sehemu kupitia ufadhili na sehemu nyingine kupitia mkopo. Tulidhani ungeleta usawa lakini umeonekana kutotosha,” alisema.
Aliongeza kuwa chini ya mfumo mpya, wazazi watakuwa na hiari ya kuchangia karo za watoto wao, lakini iwapo hawataweza kufanya hivyo, serikali itagharimia masomo yote.
“Hatutaki mwanafunzi yeyote ashindwe kuendelea na masomo kwa sababu ya ukosefu wa fedha,” alisema Rais.
Hata hivyo, maelezo ya kina kuhusu mfumo huo bado hayajatolewa.
Katibu wa Elimu ya Juu, Dkt Beatrice Inyangala, alisema pendekezo hilo bado linashughulikiwa kabla ya kuwasilishwa rasmi kwa wadau na Bunge.
“Bado tunalifafanua na kulikamilisha. Ni mchakato unaohitaji muda,” alisema.
Mwenyekiti wa Kamati ya Makamu Wakuu wa Vyuo Vikuu vya Umma, Prof Daniel Mugendi, pia alisema bado hajapokea maelezo kamili ya mfumo huo.
“Hatujapata maelezo ya kina. Yakikamilika tutashirikishwa kwa majadiliano zaidi,” alisema.
Changamoto ya ufadhili wa elimu ya juu imekuwa ikisumbua serikali kwa miaka kadhaa.
Madeni ya vyuo vikuu vya umma yameongezeka kutoka takriban Sh60 bilioni mwaka wa 2022 hadi zaidi ya Sh85 bilioni sasa.
Wakati huo huo, Mkurugenzi Mkuu wa HELB Geoffrey Monari amependekeza taasisi hiyo ipate fedha kupitia masoko ya kifedha kwa kutoa dhamana ya kijamii ya thamani ya Sh500 milioni ili kuhakikisha wanafunzi wanapata ufadhili kwa wakati.
Kwa sasa, takriban 450,000 wanaonufaika na mikopo ya HELB wanaendelea kulipa mikopo yao, hali inayowezesha bodi hiyo kukusanya karibu Sh700 milioni kila mwezi.
Mbali na mikopo, HELB hutenga Sh237 milioni kila mwaka kama ufadhili kwa wanafunzi wenye mahitaji maalumu, ambapo Sh137 milioni huenda kwa wanafunzi wa vyuo vikuu na Sh100 milioni kwa wanafunzi wa vyuo vya TVET.