Ilikuwa uongo? Helb yasema haina pesa kufadhili wanafunzi siku moja baada ahadi ya Ruto
MAELFU ya wanafunzi wanaotarajiwa kujiunga na vyuo vikuu na taasisi za mafunzo ya kiufundi (TVET) Septemba mwaka huu wako hatarini kukosa ufadhili wa serikali baada ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HELB) kutangaza kuwa inakabiliwa na upungufu mkubwa wa fedha.
Kulingana na ripoti iliyowasilishwa mbele ya Kamati ya Elimu ya Bunge la Kitaifa, HELB inahitaji Sh114.36 bilioni kufadhili wanafunzi milioni 1.2 katika mwaka wa kifedha wa 2026/2027, lakini kwa sasa ina Sh56.71 bilioni pekee. Hii inaacha pengo la Sh57.65 bilioni.
Bodi hiyo ilisema imekuwa ikikumbwa na uhaba wa fedha kwa miaka minne iliyopita huku idadi ya wanafunzi wanaohitaji msaada ikiendelea kuongezeka.
“Changamoto kubwa inayoathiri jukumu la HELB ni pengo linalozidi kupanuka kati ya fedha zinazohitajika na bajeti inayotolewa,” ilisema katika taarifa kwa wabunge.
HELB imeomba Wizara ya Fedha kuongeza fedha ili kuhakikisha wanafunzi wenye mahitaji wanaendelea kupata mikopo na ufadhili.
Bodi hiyo ilieleza kuwa kuanzishwa kwa mfumo mpya wa ufadhili wa wanafunzi mwaka 2023 kuliongeza idadi ya wanaofaidika kutoka 576,338 hadi 823,691 mwaka uliopita, hali iliyoongeza mzigo wa kifedha.
Katika mwaka wa kifedha wa 2025/2026, HELB ilipokea Sh45.66 bilioni kutoka kwa serikali na mapato yake mengine, lakini ilitumia Sh48.6 bilioni kufadhili wanafunzi.
Jumla ya wanafunzi 823,691 walipokea mikopo, huku 23,333 wakinufaika na basari na wengine 364,279 wanaosomea kozi za Sayansi, Teknolojia, Uhandisi, Hisabati, Ubunifu, Uvuvi na Kilimo wakipata ufadhili.
Haya yanajiri siku moja baada ya Rais William Ruto kutangaza kuwa wanafunzi wote watakaofuzu kujiunga na vyuo vikuu watafadhiliwa kikamilifu na serikali, hatua inayoashiria kuwa serikali inaweza kubadilisha mfumo wa ufadhili ulioanzishwa mwaka 2023 ambao umekuwa ukikosolewa na wanafunzi.