Habari za Kitaifa

Wahuni ghasia za Ol Kalou hawajashikwa timu ya DCI ikisema ‘inasubiri maagizo ya wakubwa’

Na KAMORE MAINA, WAIKWA MAINA July 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAHUNI waliozua vurugu wakati wa uchaguzi mdogo wa ubunge wa Ol Kalou bado hawajakamatwa licha ya Rais William Ruto kuagiza  maafisa wa usalama kuwasaka wahusika, hali inayozua maswali mapya kuhusu kujitolea kwa serikali kukomesha utamaduni wa kutoadhibiwa kwa wahalifu wa kisiasa.

Zaidi ya wiki moja baada ya vurugu hizo zilizogharimu maisha ya watu wawili na  makumi ya wengine kujeruhiwa, hakuna mshukiwa aliyetiwa mbaroni, licha ya picha, video na nambari za usajili za magari yanayodaiwa kutumiwa na wahuni kusambazwa mitandaoni na katika vyombo vya habari.

Timu maalumu ya Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) iliyoundwa kuchunguza vurugu hizo haikuwa imeondoka Nairobi kufikia Jumatano jioni, huku maafisa wakisema walikuwa bado wakisubiri maagizo kutoka kwa wakubwa wao.

Timu hiyo, inayojumuisha maafisa kutoka Kitengo cha Makosa Makubwa na Kitengo cha Operesheni cha DCI, iliundwa na Mkurugenzi wa DCI Mohamed Amin kuongoza uchunguzi kuhusu ghasia za uchaguzi huo.

Hata hivyo, baadhi ya maafisa waliohusika waliambia Taifa Leo kuwa bado hawajapokea maagizo ya kuelekea Nyandarua.

“Hatujapokea maagizo yoyote kutoka kwa wakubwa wetu. Bado tunasubiri,” alisema afisa mmoja wa cheo cha juu.

Kuchelewa huko kunajiri licha ya Rais Ruto kuagiza hadharani idara za usalama kuwachukulia hatua wahusika wa vurugu za kisiasa.

Akizungumza Jumatatu, Rais alisema magenge ya wahuni yanatishia demokrasia nchini na kuagiza polisi kutekeleza sheria bila upendeleo.

“Sasa kwa kuwa tumekubaliana, idara zetu usalama lazima zitekeleze wajibu wao kwa mujibu wa sheria na zikomeshe uhalifu. Hivyo ndivyo tutakavyolinda mustakabali wa Kenya,” alisema Rais Ruto.

Chini ya saa 24 baadaye, Naibu Rais Kithure Kindiki aliunga mkono kauli hiyo akisema vurugu za kisiasa sasa ni tishio kwa usalama wa taifa.

Alipokuwa akifungua rasmi Ofisi ya Usajili wa Ardhi ya Kithimani katika Kaunti ya Machakos, Profesa Kindiki aliwaonya wanasiasa dhidi ya kufadhili magenge ya wahuni.

“Haijalishi unaunga mkono serikali au upinzani. Usalama na utulivu wa taifa letu ni muhimu zaidi,” alisema.