Maoni

MAONI: Yaliyofanyika Ol Kalou yalitokea eneobunge la Kipipiri; serikali haiwezi kutuhonga sote!

Na DOUGLAS MUTUA July 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

NIMESOMA habari nyingi magazetini tangu nizaliwe, lakini kuna vichwa vichache ambavyo vimenivutia na kunata kabisa akilini mwangu: ‘Kanu Yaonja Pilipili Kipipiri’ na ‘Innocent ni Mwizi’.

Hicho cha mtu kuwa mwizi kilihusiana na kesi ambapo bwana mmoja kwa jina Innocent (hana hatia kwa Kiingereza) alikutwa na hatia ya kuiba na akahukumiwa kifungo gerezani.

Niliandika habari yenyewe nilipokuwa ripota wa mahakama, mhariri wangu akafanya kazi safi, ofisini tukaangua kicheko.

Kichwa cha Kanu kuonja pilipili kiliandikwa na gazeti hili miaka ya tisini wakati ambapo chama tawala cha wakati huo, chini ya uongozi wa marehemu Rais Daniel Moi, kilifanya juu chini kuwashawishi wapigakura kwa pesa na zawadi nono wakati wa uchaguzi mdogo katika eneobunge la Kipipiri.

Vigingi vya kusambaza umeme mashinani vilibwagwa huko, fedha nyingi kama mchanga wa baharini zikamwagwa, wakazi wakaahidiwa makuu ambayo yangepatikana tu katika ulimwengu wa kusadikika.

Hata baada ya watu kutafuna hongo kweli-kweli, walirauka siku ya uchaguzi, wakamchagua mwaniaji wa upinzani, Kanu ikaaibika, Moi akapandwa na hasira za mkizi na kuagiza vigingi hivyo vitwaliwe na kuondolewa huko kabisa!

Wenyeji hawakujali.

Amini usiamini, yaliyofanyika katika eneobunge la Ol Kalou hivi majuzi ni kisa cha historia kujirudia tu. Wakati ambapo Kanu ilionjeshwa pilipili, Ol kalou ilikuwa sehemu ya eneobunge la Kipipiri.

Kimsingi, ni sahihi kusema kuwa baadhi ya waliomkosesha Moi usingizi siku hizo ndio ambao bado wamemhangaisha Rais William Ruto na serikali yake katika uchaguzi huo mdogo uliokamilika wiki jana.

Wamedhihirisha kwamba bado wana hamu ya pesa na zawadi nyinginezo nono-nono, lakini kura zao watampigia wanayemtaka, na liwe liwalo. Hawajali wala hawabali ikiwa watawala wa nchi wataagiza baadhi ya zawadi zitwaliwe. Lengo kuu ni kumchagua wanayemtaka.

Laiti Kenya nzima ingekuwa na hulka kama ya Ol Kalou na Kipipiri. Mwananchi anayekataa kushawishiwa ili ampigie kura mtu asiyestahili anapaswa kuvuliwa kofia siku zote.

Ina maana kwamba anajua tofauti kati ya maendeleo ya kweli na hongo. Serikali ingekuwa na nia safi ingefanya maendeleo Ol Kalou mapema kabisa, hata kabla ya fursa ya uchaguzi mdogo kutokea.

Bora zaidi, Serikali ingekuwa imefanya maendeleo kama hayo katika maeneobunge yote nchini, si kusubiri wakati wa chaguzi ndogo na kukimbia kuwahonga wapigakura.

Hilo la wanasiasa kukimbia siku za mwisho limekuwa tatizo kuu nchini. Wanachaguliwa, kisha wanajificha Nairobi badala ya kuwafanyia kazi watu ambao waliwachagua.

Ukisalia mwaka mmoja au miezi kadha kabla ya uchaguzi unaofuata, wajanja hao wanarejea kwenye maeneobunge yao na kuanza kumwaga pesa kila mahali ili kuwashawishi wapigakura. Yaani mtu amekaa mbali kwa miaka minne, halafu anajitokeza ghafla na kujifanya mwokozi.

Wanafanya hata na maendeleo madogo, kisha wanawaambia wananchi wawachague tena ili wakamalize kazi walizoanzisha. Huu ni ushahidi kwamba wanamchukulia mwananchi wa kawaida kama zuzu asiyejielewa, asiye na uwezo wa kujua anahongwa.

Matokeo ya uchaguzi wa Ol Kalou – ambapo mwaniaji wa Serikali alishindwa kwa takriban kura 30,000 – yaliashiria kwamba Mkenya akitaka anaweza kujikomboa kutoka kwenye minyororo ya wanasiasa wajanja. Mbona tusifanye hivyo? Inawezekana.

Kwa tathmini za wataalamu wa masuala ya uchumi, kiasi cha pesa zilizomwagwa Ol Kalou juzi ni kikubwa hivi kwamba kila mpigakura angepata kati ya Sh148,000 na Sh150,000. Mwaka ujao Serikali itahitaji mabilioni ya fedha ili kutuhonga hivyo sote wapigakura kwa kuwa tumefikia karibu milioni 20. Hilo haliwezekani.

Unaohitajika ni uzalendo, tuipende nchi yetu, tuamue iwapo tunataka kuendelea kutawaliwa na watu wanaotuhonga na kutusababishia umaskini wa mwaka halafu. Uwezo tunao, hebu na tutie nia.

– Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika ([email protected])