Habari

DCI imefichua kuwa maafisa walilipwa kumuuwa Dkt Mutiso

Na JURGEN NAMBEKA na STEVE OTIENO August 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

WAPELELEZI wametaja Konstebo wa Polisi Elijah Kibelion Kimoi kuwa ndiye aliyempiga risasi na kumuua Daktari Victoria Mutiso katika shambulizi la kikatili lililotokea wiki iliyopita.

Idara ya Uchunguzi wa Jinai (DCI) ilisema Ijumaa kuwa Kimoi, ambaye tayari amekamatwa, alitumia bastola ya polisi kumuua Dkt Mutiso.

DCI pia ilimtaja raia Daniel Mwangi Njoroge kuwa mmoja wa waliopanga mauaji hayo.

Kulingana na DCI, Njoroge aliajiriwa na mwanasiasa Rose Mbithe Mulwa na mwanawe Christopher Mulwa kwa lengo la kumuua Dkt Mutiso.

Inadaiwa mauaji hayo yalitokana na mzozo wa muda mrefu wa kifamilia kuhusu ardhi ya ukubwa wa ekari 20 huko Mlolongo, Machakos.

Bi Mulwa amekuwa akizozania ardhi hiyo na aliyekuwa mumewe, Dkt David Musyimi Ndetei, pamoja na mkewe Dkt Mutiso tangu 2001.

Mkuu wa DCI Mohamed Amin alisema Njoroge alikodi magari mawili aina ya Toyota Prado kutekeleza mauaji hayo.

Alisema Njoroge pia alishirikiana na mhudumu wa bodaboda Kelvin Ngugi Kinuthia, ambaye anadaiwa kumsafirisha Kimoi hadi eneo la tukio na baadaye kumtorosha.

Dkt Mutiso alikuwa akisafiri katika teksi ya Uber iliyokuwa ikiendeshwa na Victor Job Chunguli mnamo Julai 29.

Walipofika eneo la Mawensi, Upper Hill, Nairobi, Toyota Prado nyeusi ilizuia teksi hiyo.Pikipiki pia ilisimama karibu nao.

Mtu aliyekuwa ameketi kiti cha nyuma cha pikipiki alifyatua risasi kadhaa kuelekea Dkt Mutiso kabla ya pikipiki na Prado kutoroka.

Bw Chunguli alimpeleka Dkt Mutiso katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta, lakini akatangazwa kuwa amefariki alipowasili.

Bw Amin alisema baada ya kuwahoji Njoroge na Kinuthia, wawili hao waliwapeleka wapelelezi kwa maafisa watatu wa polisi.

Walitajwa kuwa Inspekta Kenneth Kipkemboi Sang, Konstebo Elijah Kibelion Kimoi na Konstebo Collins Kiplangat Bett.

Kimoi amekamatwa huku Sang na Bett wakitoroka na wanaendelea kusakwa na polisi

.
“Kushiriki kwa maafisa hawa ni usaliti mkubwa kwa sare ya polisi na imani ambayo umma umeweka kwao. Lazima wachukuliwe hatua,” alisema Bw Amin.

Bw Amin pia alisema bastola iliyotumiwa kumuua Dkt Mutiso ilikuwa ya polisi na ilikuwa imewekwa katika kituo kidogo cha polisi cha Nderi, chini ya Kituo cha Polisi cha Kikuyu.

Wapelelezi walipokagua sanduku la kuhifadhia silaha katika kituo hicho, walipata bastola aina ya Mini Jericho yenye nambari KP47302127 pamoja na magazini iliyokuwa na risasi 12 za milimita tisa.

Ukaguzi wa rejista ya utoaji wa silaha ulionyesha kuwa bastola hiyo ilikuwa imetolewa kwa Inspekta Sang.

Silaha hiyo ilipelekwa katika maabara ya uchunguzi wa kisayansi ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi kwa uchunguzi wa risasi.

Kulingana na DCI, uchunguzi ulithibitisha kuwa bastola hiyo ndiyo iliyotumiwa katika kumuua Dkt Mutiso.

Maganda ya risasi yaliyopatikana eneo la tukio na kichwa cha risasi kilichopatikana mwilini mwa marehemu wakati wa uchunguzi wa mwili vililingana na risasi kutoka kwa bastola hiyo.

Bastola hiyo pamoja na pikipiki ya Kinuthia zimechukuliwa na polisi kama ushahidi.

Uchunguzi wa mauaji hayo ulihusisha pia kuangalia picha za kamera za usalama, ushahidi wa kisayansi na taarifa nyingine za kijasusi.

 

DCI ilisema ushahidi uliopatikana unaonyesha kuwa baadhi ya washukiwa wa mauaji ya Dkt Mutiso huenda pia walihusika katika mauaji ya wakili Kyalo Mbobu mnamo Septemba 9, 2025.

Mbobu alipigwa risasi na mtu aliyekuwa nyuma ya pikipiki akiendesha gari kuelekea nyumbani kando ya Barabara ya Magadi.

Mauaji hayo yalifanana na yaliyompata Dkt Mutiso kwa kuwa mshambuliaji alitumia pikipiki.

Bw Amin pia alidai kuwa matamshi ya Naibu Rais wa zamani Rigathi Gachagua kuhusu uchunguzi huo huenda yalifikia Sang na Bett na kuwafanya kutoroka.

Alimtaka Bw Gachagua kuwasilisha kwa DCI taarifa yoyote aliyo nayo ambayo inaweza kusaidia uchunguzi wa mauaji hayo.

Bw Gachagua alikuwa amedai kuwa maafisa wawili wa polisi kutoka Kituo cha Polisi cha Kikuyu walihusika katika mauaji ya Dkt Mutiso.

Alisema madai yake yalitokana na “taarifa za kuaminika”.
“Maafisa hawa wawili katika Kituo cha Polisi cha Kikuyu ndio waliomuua wakili Kyalo Mbobu na pia Dkt Victoria Mutiso,” Bw Gachagua alisema.