Doreen Nabwire, Wanawake walipwe sawa na wanaume
Nahodha wa zamani wa Harambee Starlets Doreen “Dodo” Nabwire amesema inawezekana, wachezaji wa soka wa kike kulipwa sawa na wanaume mradi wadau wa mchezo huo wajitolee kukuza soka ya wanawake.
Nabwire, ambaye aliweka historia kuwa Mkenya wa kwanza kucheza soka ya kulipwa Ulaya, aliyasema hayo katika mahojiano ya kipekee na Taifa Spoti kwenye Ofisi ya Kanda ya Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) iliyoko katika Kituo cha Soka cha Mohammed VI mjini Salé, Morocco.
Ofisi ambayo iliyofunguliwa Julai 26 mwaka jana, ndiyo kitovu cha FIFA kinachoratibu shughuli za kiufundi na kiutawala kwa mashirikisho ya soka barani Afrika. Nabwire sasa amehamia nchini Morocco na familia yake.
Kwa sasa Nabwire anahudumu kama Kiongozi wa Soka ya Wanawake wa FIFA barani Afrika. Anasema licha ya mchezo huo kupiga hatua kubwa, bado wachezaji wa kike wanabaguliwa katika malipo na kutambuliwa.
“Hatutaki kuwa wanaume. Tunapenda mchezo huu na tunataka uheshimiwe kama ulivyo wa wanaume. Tuwezeshwe kuonyesha vipaji vyetu na kutimiza ndoto zetu. Soka ya wanawake inaendelea kukua,” alisema.
Aliipongeza Shirikisho la Soka Kenya (FKF) kwa kuweka misingi iliyochangia maendeleo ya soka ya wanawake, ingawa alisisitiza kuwa kuna haja ya kuongeza uwekezaji.
“Katika kipindi cha aliyekuwa rais wa FKF Nick Mwendwa tuliweka mikakati ya kuimarisha soka ya wanawake. Ligi ya wanawake iliandaliwa kwa mfumo unaofanana na ule wa wanaume na tulinuia kuhakikisha inapata usaidizi sawa. Hata hivyo, bado tunalazimika kujikumbusha na kuomba tutambuliwe. Taratibu mambo yanabadilika,” alisema.
Nabwire alisema mafanikio makubwa ambayo Kenya imepata kimataifa yametokana zaidi na soka ya wanawake.
“Timu ya wasichana chini ya umri wa miaka 17 imecheza Kombe la Dunia, Harambee Starlets imefuzu kwa Kombe la Mataifa ya Afrika (WAFCON) kwa juhudi zao wenyewe.”
Alitaja Marekani na Uswidi kama baadhi ya mataifa ambayo yamefanikiwa kupigania malipo sawa kwa wanasoka wa kike na wa kiume.
“Wanawake wanafanya mazoezi sawa, wanatumia muda sawa uwanjani na wanajitolea kama wanaume. Kwa nini wasilipwe sawa? Inawezekana. Kinachohitajika ni dhamira na uwekezaji zaidi,” alisema.
Aliongeza kuwa kuongeza uwekezaji, wadhamini na kuipa soka ya wanawake nafasi kubwa kwenye vyombo vya habari kutasaidia kupunguza pengo lililopo kati ya mchezo wa wanaume na wanawake.
Mama huyo wa watoto watatu aliandika historia mwaka 2009 alipokuwa Mkenya wa kwanza kucheza soka ya kulipwa Ulaya baada ya kutua Werder Bremen ya Ujerumani.
Katika mechi yake ya kwanza ya ligi mnamo Septemba 27, alifunga mabao mawili dhidi ya Hamburger SV II katika sare ya 2-2 na kuwa mchezaji wa kwanza kufunga mabao kwa Werder Bremen ya Ligi Daraja la Pili. Alifunga jumla ya mabao saba katika mechi 18 alizoichezea klabu hiyo ndani ya msimu mmoja.