Habari za Kitaifa

Yangu na yako yameishia hapa, Gavana Mutai amtema naibu wake

Na VITALISI KIMUTAI August 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MWAKA mmoja kabla ya Uchaguzi Mkuu wa Agosti 10, 2027, Gavana wa Kericho Erick Mutai, ametangaza wazi mwisho wa ushirikiano wake wa kisiasa na Naibu Gavana Fred Kirui, akihitimisha uhusiano ambao umekuwa na misukosuko ya kisiasa na kiutawala kwa miaka minne iliyopita.

Akizungumza katika wadi ya Chilchila, eneo bunge la Kipkelion West, Dkt Mutai alisema hadharani kuwa amempa Bw Kirui uhuru wa kutafuta mshirika mwingine wa kisiasa kuelekea uchaguzi ujao, iwe kama mgombea wa ugavana au mgombea mwenza.

Gavana huyo alidai kuwa Naibu wake alihusika na majaribio yaliyotibuka ya kumng’atua madarakani.

Alisema sasa ataungana kisiasa na aliyekuwa Mbunge wa Kipkelion, Bw Jackson Rop, ambaye kwa sasa ni Waziri wa Kaunti anayesimamia Fedha na Mipango ya Kiuchumi.

“Uhusiano wetu wa kisiasa umefikia mwisho. Kuanzia sasa nitafanya kazi na Jackson Rop na nitatafuta muhula wa pili nikiwa na mgombea mwenza mpya,” alisema Dkt Mutai.

Kwa upande wake, Mhandisi Kirui alimshutumu gavana kwa kumdhalilisha na kutomheshimu tangu walipochaguliwa mwaka 2022. Alisema hali hiyo imefanya ushirikiano wao usiwezekane.

“Wananchi wa Kipkelion West wataamua mwelekeo wao wa kisiasa mwaka 2027 kutokana na namna ulivyonitendea licha ya kutupatia kura kwa wingi,” alisema Kirui.

Mzozo kati ya viongozi hao unadaiwa kuchochewa na makubaliano ya kugawana madaraka kwa uwiano wa asilimia 60 kwa gavana na asilimia 40 kwa naibu wake, madai ambayo Dkt Mutai amekuwa akikanusha.

Tofauti zilianza mara tu baada ya kuapishwa kwao wakati wa uteuzi wa Mawaziri wa Kaunti na maafisa wakuu, ambapo Kirui alidai hakushirikishwa.

Huku uchaguzi wa 2027 ukikaribia, kinyang’anyiro cha ugavana Kericho kinaonekana kuwa na ushindani mkali, huku Charles Keter, Florence Bore na Spika wa Bunge la Kaunti Dkt Patrick Mutai wakitajwa miongoni mwa wanaotaka kuwania.