Serikali yatetea mageuzi katika sekta ya afya licha ya changamoto
SERIKALI imetetea mageuzi yake katika sekta ya afya, ikisema imetekeleza ahadi nyingi ilizotoa wakati wa kampeni licha ya changamoto mbalimbali.
Rais William Ruto alisema maendeleo katika sekta ya afya hayapaswi kupimwa kwa idadi ya sheria zilizopitishwa au watu waliosajiliwa pekee, bali kwa uzoefu wa mgonjwa anayepata huduma.
“Kipimo halisi cha mafanikio ni ikiwa mgonjwa anapata huduma za afya zinazotegemewa, nafuu na zenye kuheshimu utu wake,” alisema Rais.
Alizungumza wakati wa Kongamano la kwanza la Kitaifa la Afya nchini Kenya lililoandaliwa na Wizara ya Afya chini ya kaulimbiu “Mageuzi yamewasilishwa, Afya ni Haki”, ambalo linalenga kujadili changamoto na mafanikio ya sekta hiyo.
Rais alisema alipoingia mamlakani, mojawapo ya vipaumbele vyake vilikuwa kufufua mpango wa Huduma ya Afya kwa Wote (UHC), ambao alihisi ulikuwa umedorora.
Hivyo, UHC ikawa moja ya nguzo tano za Ajenda ya Mabadiliko ya Kiuchumi kutoka Chini kwenda Juu.
Kwa mujibu wake, maradhi yanaweza kufilisi familia na kuwafanya wananchi kuingia katika umaskini, jambo lililomsukuma kutunga sheria nne mpya za afya mwaka 2023 zilizozaa Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA).
Kati ya Wakenya milioni 32.3 waliosajiliwa chini ya SHA, zaidi ya milioni nane wamepokea huduma za matibabu.
Idadi hiyo inajumuisha akina mama milioni 1.2 waliosaidika kujifungua salama na zaidi ya 500, 000 kwa upasuaji tangu mpango huo uanzishwe.
Rais alipuuziliaa mbali madai kwamba ameacha ajenda ya “hasla”, akisema ana ushahidi kuwa wananchi wa kipato cha chini ndio wanufaika wakubwa wa SHA.
“Haya si mageuzi ya siku moja. Ni safari endelevu ya kupunguza pengo kati ya ahadi tulizotoa na huduma anayopokea kila Mkenya,” alisema.
Hata hivyo, wadau wa afya walihoji kuwa licha ya maendeleo yaliyopatikana katika sera, changamoto kubwa bado ipo katika utekelezaji.
Mkurugenzi Mkuu wa Reproductive Health Network Kenya, Bi Nelly Munyasia, alisema Kenya imepiga hatua katika sera za afya ya uzazi, lakini huduma hizo hazijafikishwa kikamilifu kwa wananchi.
“Baadhi ya sera bora zaidi zinasalia kwenye makaratasi kwa sababu rasilimali hazijaelekezwa ipasavyo ili kuzitekeleza,” alisema.
Alisisitiza umuhimu wa ufadhili endelevu, miundombinu ya kutosha, wafanyakazi wenye ujuzi na mifumo bora ya rufaa za wagonjwa.
Kwa upande wake, Patrick Oyaro wa mradi wa Liverpool VCT and Research Kenya (LVCT), alisema huduma za watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi zinapaswa kujumuishwa kikamilifu chini ya SHA.
“Kwa muda mrefu huduma za Ukimwi zimefadhiliwa na wafadhili. Tunahitaji kubadili hali hiyo na kuhakikisha zinaingizwa kwenye SHA,” alisema.
Kongamano hilo linafanyika wakati ambapo nchi inashuhudia mgomo wa wahudumu wa afya wa UHC na wauguzi.
Mwenyekiti wa Muungano wa Maafisa wa Utabibu Kenya, Peterson Wachira, alisema Kenya bado iko mbali na malengo ya Ruwaza ya 2030 ya kuwa kitovu cha utalii wa matibabu barani Afrika.
Aliongeza kuwa nchi pia haijafikia Azimio la Abuja linalotaka asilimia 15 ya bajeti ya taifa kutengewa sekta ya afya.
“Mfumo wa usimamizi wa wahudumu katika afya umegawanyika mno. Upendeleo na ufisadi zimekithiri na wafanyakazi wengi wa afya wanateseka kutokana na uchovu na msongo wa mawazo,” alisema.
Naye Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Madaktari, Wafamasia na Madaktari wa Meno (KMPDU), Dkt Dennis Miskella, alisema changamoto kubwa inayopuuzwa ni masuala ya wafanyakazi wa afya.
“Kaunti zaidi ya 40 bado hazijalipa mishahara ya madaktari. Tunahitaji mjadala wa kina kuhusu uongozi na usimamizi wa sekta hii,” alisema.
Alipendekeza kuwa magavana washughulikie huduma za msingi za afya huku serikali kuu ikisimamia huduma za matibabu ya kiwango cha juu ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.