Afya na Jamii

Athari za dawa za kufisha ganzi wakati wa kujifungua kwa upasuaji

Na WINNIE ONYANDO August 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 4

KWA Atieno, kumbukumbu ya siku aliyomkaribisha kifungua mimba wake duniani haikujumuisha tu furaha ya kumwona mwanawe, bali pia hofu aliyokuwa nayo kabla ya kujifungua kwa upasuaji (Caesarean Section).

Alipofahamishwa kuwa angelazimika kujifungua kwa upasuaji, jambo lililomtisha zaidi halikuwa upasuaji wenyewe bali sindano ya kufisha ganzi inayodungwa kwenye uti wa mgongo.

Alikuwa amesikia kutoka kwa marafiki kwamba dawa hiyo inaweza kusababisha maumivu ya kudumu ya mgongo, kupooza au hata matatizo ya kumbukumbu baadaye.

“Nilikuwa na hofu sana. Nilijiuliza kama baada ya kujifungua ningebaki na matatizo ya mgongo au kama dawa hiyo ingeathiri afya yangu miaka ya baadaye,” anasema.

Utaratibu wa kufisha ganzi

Hata hivyo, baada ya kuelekezwa na wataalamu wa afya kuhusu jinsi utaratibu wa kufisha ganzi unavyofanya kazi na kwa nini ilikuwa inafaa katika hali yake, hofu yake ilianza kupungua.

Kulingana na Shirika la Kitaifa la Takwimu Nchini (KNBS), uzazi kwa njia ya upasuaji nchini umefikia asilimia 20.1 ya jumla ya uzazi unaofanyika katika vituo vya afya, hatua inayomaanisha kuwa zaidi ya mmoja kati ya kila watoto watano huzaliwa kwa upasuaji.

Idadi hiyo imevuka kiwango cha juu cha asilimia 15 kinachopendekezwa na Shirika la Afya Duniani (WHO).

Kisa kama cha Atieno kinaweza kuwa cha kawaida kwa wanawake wengi wanaofaa kufanyiwa upasuaji wa aina hiyo, huku baadhi yao wakiamini kwamba dawa za kufisha ganzi uti wa mgongo au nusukaputi zinazotumiwa wakati wa upasuaji zinaweza kubaki mwilini na kusababisha matatizo ya kudumu.

Lakini wataalamu wanasema kuna tofauti kubwa kati ya hofu kuhusu ganzi na kile ambacho sayansi ya tiba inaonyesha.

Kulingana na Dkt Ong’ech Odero John, daktari wa akina mama katika hospitali ya Nairobi Reproductive Health Services ambaye amekuwa katika taaluma hiyo kwa zaidi ya miaka 23, aina ya ganzi inayotumiwa wakati wa upasuaji huo huamuliwa kulingana na hali ya mama, mtoto na mazingira ya upasuaji.

“Kwa upasuaji mwingi uliopangwa na hata dharura, kufisha ganzi uti wa mgongo au nusukaputi ndiyo hupendelewa iwapo hakuna sababu ya kimatibabu inayozuia matumizi yake,” anasema.

Kwa wale wanaodungwa aina hiyo ya dawa kwenye uti wa mgongo, (spinal anaesthesia), kiasi kidogo cha dawa ya kuondoa maumivu hudungwa kwenye majimaji yanayozunguka neva katika sehemu ya chini ya mgongo.

Sehemu ya chini ya mwili huwa ‘imekufa’ kwa muda na mama kwa kawaida hubaki macho wakati wa upasuaji.

Hii humwezesha mama kuwa macho wakati mtoto anazaliwa, huku maumivu ya upasuaji yakizuiwa.

Utaratibu wa nusukaputi

Kwa baadhi ya wanawake, uwezo wa kuwa macho na kumsikia mtoto akilia kwa mara ya kwanza pindi tu anapozaliwa ni mojawapo ya faida kubwa za aina hii ya dawa.

Pia, kwa kawaida haihitaji kuwekwa mrija wa kupitisha hewa kwenye koo, jambo ambalo ni tofauti na utaratibu wa nusukaputi (general anaesthesia).

“Faida nyingine ni kwamba kiwango cha dawa kinachomfikia mtoto huwa kidogo sana, na kwa kutumia dawa inayofaa ya kupunguza maumivu, uti wa mgongo unaweza pia kusaidia kutoa unafuu wa maumivu baada ya upasuaji,” anasema Dkt Ong’ech.

Hata hivyo, kufisha ganzi uti wa mgongo kuna madhara yake.

“Shinikizo la damu la mwathiriwa linawezakushuka, mama anaweza kusikia kichefuchefu, kutetemeka au kuwashwa mwilini,” anaeleza Dkt Ong’ech.

Shinikizo la damu, Dkt Ong’ech anasema, hufuatiliwa kwa karibu wakati wote wa upasuaji na linaweza kutibiwa kwa haraka kwa kutumia maji ya mishipa au dawa.

Pia kuna madhara ambayo hayatokei mara nyingi, kama vile maumivu makali ya kichwa, sehemu za mwili kutofanya kazi ipasavyo na hivyo kuhitaji dawa zaidi au kubadilishwa kuwa nusukaputi.

Katika hali nadra zaidi, kunaweza kutokea maambukizi, kutokwa damu karibu na neva za uti wa mgongo, kuumia kwa neva au mzio mkali wa dawa.

Kwa upande mwingine, nusukaputi humfanya mgonjwa kupoteza fahamu wakati wa upasuaji. Dawa hutolewa ili kumfanya mama alale, na kwa kawaida mrija huwekwa kwenye njia ya hewa huku mashine ikimsaidia kupumua wakati wa upasuaji. Baada ya dawa kuanza kuisha nguvu, mama huanza kuamka.

Dkt Ong’ech anasema nusukaputi ni muhimu sana katika hali fulani na si sahihi kwa mwanamke kuamini kwamba aina hii ya ganzi ni hatari kila wakati.

“Inaweza kutumika wakati upasuaji ni wa dharura kiasi kwamba hakuna muda wa kutosha kufisha ganzi uti wa mgongo au wakati kufisha ganzi uti wa mgongo hakuwezi kutumiwa,” anaeleza daktari huyo.

Pia utaratibu huo unaweza kuhitajika mama akiwa anatokwa na damu nyingi, ana matatizo makubwa ya moyo na mishipa, ana tatizo la kuganda kwa damu au anatumia dawa za kupunguza kuganda kwa damu.

“Nusukaputi pia ni mbinu salama na muhimu inapohitajika. Hasa katika hali za dharura, inaweza kuokoa maisha,” anasema.

Je, dawa hubaki mwilini?

Mojawapo ya hofu zinazowasumbua baadhi ya wanawake ni kwamba dawa inaweza kubaki mwilini kwa miaka mingi na kusababisha matatizo ya kumbukumbu, akili au afya ya uzazi.

Dkt Ong’ech anasema ni muhimu wanawake kupata maelezo kutoka kwa wataalamu badala ya kutegemea simulizi za watu.

Anasema aina ya dawa huzingatia hali ya kila mgonjwa na aina ya upasuaji unaofanywa.

Kwa hivyo, mwanamke aliyekufishwa ganzi uti wa mgongo hapaswi kudhani kwamba kwa sababu alipokea aina hiyo ya upasuaji, dawa hiyo itaendelea kuwa mwilini na kumletea matatizo miaka ijayo.

Vipi kuhusu uti wa mgongo?

Hofu nyingine maarufu ni kwamba sindano ya kufisha ganzi hasa inayodungwa kwenye uti wa mgongo inaweza kusababisha maumivu ya mgongo ya kudumu au hata kupooza.

Ingawa matatizo ya neva ni miongoni mwa madhara yanayoweza kutokea, Dkt Ong’ech anasema matatizo makubwa ni nadra.

Kabla ya kudungwa dawa, daktari huangalia historia ya afya ya mama mjamzito, dawa anazotumia na hali nyingine zinazoweza kuongeza hatari.

“Hii ndiyo sababu wanawake wanashauriwa kumweleza daktari husika kuhusu dawa zote wanazotumia, hasa dawa za kupunguza kuganda kwa damu,” anasisitiza daktari huyo.

Pia anasema waathiriwa wanapaswa kumweleza daktari iwapo wana matatizo ya kuganda kwa damu, idadi ndogo ya chembechembe za damu, matatizo ya mgongo, wamewahi kufanyiwa upasuaji wa uti wa mgongo au wana ugonjwa wa neva.

Kwa mama mjamzito, usalama wa mtoto ni sehemu muhimu ya uamuzi kuhusu aina ya upasuaji.

Kwa kufisha ganzi uti wa mgongo, mama huwa macho na kiwango cha dawa kinachomfikia mtoto kwa kawaida huwa kidogo.

Kwa nusukaputi, dawa hupitia kwenye kondo la nyuma na zinaweza kumfikia mtoto.

Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba aina hiyo ya upasuaji ni hatari kwa kila mtoto.

Aina hiyo inaweza kuwa muhimu katika hali ambapo kuchelewesha upasuaji ili kutumia njia mbadala kunaweza kuhatarisha maisha ya mama au mtoto.

“Kwa hivyo, uamuzi haupaswi kufanywa kwa kuogopa jina la dawa bali kwa kuzingatia hali halisi ya mama na mtoto wakati huo.”

Kwa mujibu wa Dkt Ong’ech, mojawapo ya mambo muhimu zaidi ambayo mama anaweza kufanya ili kupunguza hatari ni kumpa daktari taarifa kamili kuhusu afya yake.

“Hii inahusisha dawa zote anazotumia, tatizo alilowahi kuwa nalo, matatizo aliyowahi kupata kutokana na ganzi, matatizo ya kuganda kwa damu, magonjwa ya moyo au mapafu na muda aliokula au kunywa mara ya mwisho.

Pia mama anapaswa kueleza hofu na mapendeleo yake.

“Usiogope kuuliza kuhusu aina ya dawa, kwa nini imechaguliwa na madhara yanayoweza kutokea,” anashauri.