Habari

Tiketi ya Sifuna–Kalonzo yaendelea kupigiwa debe

August 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UCHAGUZI Mkuu wa 2027 unapokaribia, upinzani unaanza kuashiria mwelekeo wa kuungana na vuguvugu la Linda Mwananchi, huku mjadala kuhusu nani atabeba bendera ya urais ukizidi kupamba moto.
Katika ishara ya mwelekeo huo, Seneta wa Kakamega Boni Khalwale ameibua uwezekano wa tiketi ya Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na Kalonzo Musyoka, akidai kuwa muungano huo unaweza kupatia upinzani nafasi nzuri ya kumkabili Rais William Ruto.
Bw Khalwale alisema Ijumaa kwamba utafiti aliouhusisha na wasomi kutoka China unatabiri kuwa Sifuna akiwa mgombea wa urais na Kalonzo mgombea mwenza, wanaweza kupata asilimia 68 ya kura dhidi ya asilimia 29 ya Rais Ruto.
“Nimesoma utafiti jana usiku ambao umefanywa na Wachina. Umesema kwamba sisi tulioko mrengo wa upinzani tukikufanya wewe kuwa mgombea urais, halafu Kalonzo Musyoka awe mgombea mwenza wako, wewe na Kalonzo mtapata asilimia 68 ya kura, huku William Ruto akienda Sugoi na asilimia 29, ” alidai Khalwale.
Hata hivyo, Khalwale hakutaja taasisi iliyofanya utafiti huo, ulifanywa lini, sampuli iliyotumika au mbinu iliyotumiwa. Hakuna ripoti ya utafiti huo iliyowekwa wazi ili kuthibitisha takwimu hizo.
 Licha ya utata huo, kauli yake inaangazia hesabu inayozidi kutawala siasa za upinzani: je, Sifuna anaweza kuwa sura ya kizazi kipya cha upinzani huku Kalonzo akitoa uzoefu na ukomavu wa kisiasa?
 Sifuna amekuwa akipanda katika kura za maoni na sasa anatajwa miongoni mwa viongozi wanaoweza kupewa nafasi ya kuongoza upinzani.
 Utafiti wa TIFA uliotolewa Julai ulimweka Rais Ruto mbele kwa asilimia 24, Sifuna akifuata kwa asilimia 15 na Kalonzo akiwa na asilimia 13.
 Uchaguzi wa Kenya huamuliwa pia na miungano ya kikanda, nguvu za vyama, wagombea wenza na uwezo wa kuvutia wapiga kura nje ya ngome za viongozi.
Kwa Sifuna, changamoto ni kugeuza umaarufu wake unaokua kuwa mtandao wa kitaifa. Kwa Kalonzo, changamoto inaweza kuwa kuamua ikiwa yuko tayari kuachana na azma ya kuwania urais na kukubali kuwa mgombea mwenza.
Mjadala huo unajiri huku viongozi wa Linda Mwananchi wakiongeza shughuli za kisiasa na baadhi ya viongozi wa upinzani wakionyesha wako tayari kufanya kazi nao.
Hata hivyo, bado hakuna makubaliano rasmi kuhusu mgombea wa upinzani, chama kitakachotumika au nafasi ya Kalonzo katika mpangilio huo.
Kwa hivyo, tiketi ya Sifuna na Kalonzo bado ni uvumi wa kisiasa kuliko mpango uliokamilika.
Lakini mjadala wake unaonyesha mabadiliko yanayoendelea katika upinzani huku 2027 ikikaribia: kutoka mashindano ya mtu mmoja mmoja hadi kutafuta tiketi moja inayoweza kuunganisha nguvu za kisiasa kutoka maeneo mbalimbali ya nchi.
 Iwapo Linda Mwananchi itaungana rasmi na makundi mengine ya upinzani, suala la nani atakuwa mgombea wa urais na nani atakuwa mgombea mwenza litakuwa mojawapo ya maamuzi magumu zaidi kuelekea uchaguzi huo.
Kwa sasa, jina la Sifuna limeingia katika hesabu hiyo. Kalonzo ana uzoefu na ngome yake ya kisiasa.
Swali kubwa ni ikiwa wawili hao wanaweza kugeuza nguvu zao kuwa muungano mmoja wenye mvuto wa kitaifa — na ikiwa viongozi wengine wa upinzani wako tayari kuunga mkono mpango huo.