Tahadhari pombe feki ikitamba nchini
YOTE huanza kwa chupa ya pombe ya bei nafuu, chapa inayofahamika au kinywaji kilichonunuliwa katika baa inayoaminika. Kisha huja ladha ya ajabu, kuwasha koo, kutapika, kushindwa kuamka au hata madhara mabaya zaidi.
Kote nchini Kenya, watumiaji wa pombe wanaeleza visa vya kunywa vileo wanavyoshuku kuwa ni bandia au vilivyotiwa kemikali hatari. Baadhi yao waliishia hospitalini, wengine wameogopa kunywa tena huku wengine wakibadilisha kabisa aina ya pombe wanazotumia.
Visa hivyo vinaendelea kuibuka katika maeneo mbalimbali nchini na hata kusambaa kwenye mitandao ya kijamii huku mamlaka zikijitahidi kudhibiti tatizo hilo.
Wiki hii pekee, maafisa kutoka mashirika mbalimbali walinasa mamia ya chupa za pombe zinazoshukiwa kuwa bandia katika maeneo ya Eastleigh na Jericho jijini Nairobi. Operesheni hiyo pia ilifanikisha kukamatwa kwa stampu za ushuru zinazoshukiwa kuwa feki, chupa tupu na vifuniko vya chupa.
Katika mtaa wa Eastleigh, jumla ya chupa 868 za vinywaji mbalimbali zilinaswa, huku 315 zikipatikana Jericho.
Ripoti ya utafiti mwaka 2025 iliyochapishwa na Mamlaka ya Kupambana na Bidhaa Bandia (ACA) ilionya kuwa sekta ya vinywaji vya kileo inakabiliwa na changamoto kubwa ya bidhaa ghushi zinazohatarisha afya ya watumiaji na uadilifu wa soko.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, divai ndiyo bidhaa inayoghushiwa zaidi kwa asilimia 50.12, ikifuatiwa na bia kwa asilimia 47.44. Mvinyo ulirekodi asilimia 42.68 huku vodka ikifikia asilimia 36.95.
John Kamau, mkazi wa Kiambu, anasimulia jinsi alivyokumbwa na matatizo makubwa baada ya kunywa pombe katika baa moja katikati mwa Nairobi.
“Pombe ilikuwa chungu kupita kiasi. Niliendelea kuinywa kwa sababu nilikuwa tayari nimelipia. Asubuhi iliyofuata nilipatwa na maumivu makali ya kichwa, tumbo kuuma na kutapika mara kwa mara. Hata kufikia Jumatatu sikuweza kwenda kazini,” alisema.
Kamau alisema alitumia takriban Sh3,000 hospitalini kununua dawa na tangu wakati huo ameamua kuacha pombe kabisa.
Mark Pollard, mshauri wa biashara kutoka Australia ambaye amekuwa akifikiria kuhamia Kenya, alisema alitapika na kuharisha mara mbili katika mazingira yanayomfanya ashuku pombe bandia.
“Mara ya pili nilikuwa nimekunywa kiasi kidogo sana cha kileo nilichonunua kutoka duka maarufu. Ndani ya muda mfupi nilianza kutapika na kuharisha kupita kiasi,” alisema.
Hata hivyo, alikiri kuwa hawezi kuthibitisha kwa asilimia mia moja kwamba pombe ndiyo ilisababisha matatizo hayo kwa kuwa huenda kulikuwa na sababu nyingine za kiafya au chakula.
Mfanyabiashara na mwandishi wa masuala ya kitaaluma Robert Ouko Owino alisema tukio lake lilitokea Juni.
“Sikuweza kufanya kazi kwa siku tatu. Nimewahi kunywa pombe nyingi hapo awali lakini nilijua hali hii ilikuwa tofauti kabisa na kawaida,” alisema.
Kwa mujibu wake, watu wengi waliowasiliana naye baada ya kuandika kuhusu suala hilo walisimulia walivyolazwa hospitalini na kupata matatizo ya ini au kongosho (pancreas).
Jeremiah Kinuthia, mwenye umri wa miaka 28 kutoka Nairobi, alisema alilazwa katika Hospitali ya Karen baada ya kunywa pombe iliyokuwa na ladha tofauti na ile aliyozoea.
“Nilianza kutokwa na jasho na kupata shida ya kupumua. Nililazimika kuwekewa maji mwilini hospitalini,” alisema.
Tangu tukio hilo, ameacha kutumia pombe kali na sasa hunywa bia pekee.
Dkt Joseph Wahome Mukundi, mtaalamu wa sumu katika Hospitali ya Rufaa na Mafunzo ya Meru, alisema kemikali inayohusishwa mara nyingi na pombe bandia ni methanol, ambayo hutumika viwandani.
Alieleza kuwa methanol hubadilika mwilini kuwa kemikali hatari zinazoweza kusababisha upofu, kuharibika kwa figo, kushindwa kwa viungo vya mwili na hata kifo.
“Mishipa ya macho inaweza kuathirika na kusababisha upofu ikiwa mtu hatapata matibabu ya haraka,” alisema.
Daktari huyo amewataka watengenezaji wa pombe kutumia teknolojia kama misimbo ya QR ili kuwasaidia wanunuzi kuthibitisha uhalisi wa bidhaa.
Pia amewahimiza Wakenya kununua pombe katika maduka makubwa na maeneo yaliyoidhinishwa rasmi ili kurahisisha ufuatiliaji iwapo kutatokea matatizo.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa ACA Robi Mbugua alisema bei ya chini isiyo ya kawaida inapaswa kuwa ishara ya tahadhari kwa wanywaji.