Kalonzo avamia ngome ya Ruto Taita Taveta na kutumia mzozo wa ardhi kumshambulia
VIONGOZI wa upinzani Jumamosi walivamia Taveta, eneo linalotajwa kuwa ngome ya kisiasa ya Rais William Ruto, wakitumia mzozo wa ardhi na madai ya kufurushwa kwa wakazi kuishambulia serikali.
Msafara huo uliongozwa na kiongozi wa Wiper Patriotic Front, Kalonzo Musyoka, Ulifika Mkocheni, karibu na shamba la Rais Ruto la Eldoro, ambako familia kadhaa zilizofurushwa takriban mwaka mmoja uliopita bado zinaishi katika kambi.
Viongozi hao walishutumu serikali kwa madai ya kutumia maafisa wakuu kuwaondoa wananchi kwenye ardhi na kuwaacha bila makao.
Katika msafara huo walikuwa kiongozi wa Democratic Party, Justin Muturi, kiongozi wa DAP-Kenya, Eugene Wamalwa, aliyekuwa Waziri wa Utumishi wa Umma, Aisha Jumwa, Mbunge wa Wundanyi ,Danson Mwashako na zaidi ya wabunge 20.
Bw Musyoka aligeuza mzozo huo kuwa shambulizi kali dhidi ya Rais Ruto, akidai Rais alinunua takriban ekari 2,000 kutoka kwa mfanyabiashara Basil Criticos lakini baadaye akaongeza eneo hilo, hatua aliyosema imewaacha wenyeji bila makao.
“Rais aliuziwa ekari 2,000 pekee na Basil Criticos lakini ameongeza, na kuwaacha wenyeji bila makao,” alisema Bw Musyoka.
Pia alikosoa matumizi ya fedha za umma kujenga barabara zinazoelekea katika shamba la Rais, akisema rasilimali za serikali zinafaa kuwanufaisha wananchi.
“Leo tumeshangaa kuona Ikulu nyingine ikijengwa Taveta kwa gharama ya watu wa Taveta,” alisema.
Bw Muturi naye alitoa madai mazito akisema alipokuwa Mwanasheria Mkuu aliidhinisha stakabadhi za kuharakisha ujenzi wa barabara Taveta bila kujua kuwa zingemfaidi Rais moja kwa moja.
“Ningejua stakabadhi nilizokuwa nikitia saini zingemfaidi Rais moja kwa moja, ningechukua hatua tofauti,” alisema.
Wakati huo huo, wakazi wa Jipe wamekuwa wakitaka ua unaozunguka ardhi yenye mzozo kuondolewa kufuatia uamuzi wa Mahakama ya Mazingira na Ardhi uliowaunga mkono.
Wakazi hao wanadai ekari 3,000 zilitolewa kwa mpango wa Jipe-Taveta Settlement kuwawezesha maskwota kupata ardhi.
Sasa wanataka serikali kutekeleza uamuzi wa mahakama, kuwarejesha waliofurushwa na kuwapa hatimiliki ili kumaliza mzozo huo wa miaka mingi.
Kalonzo alimlaumu rais kwa kushindwa kukabili gharama ya maisha na kuongezeka kwa umaskini nchini.
Bw Musyoka alisema serikali ya Kenya Kwanza imekuwa ikitumia vitisho, pesa na ahadi za kisiasa kuwavutia viongozi wa upinzani kwa lengo la kuimarisha nafasi ya Rais Ruto kuelekea uchaguzi ujao.
Aliwashutumu viongozi wa serikali kwa kujaribu kudhoofisha upinzani kwa kuwashawishi wabunge, maseneta na magavana kujiunga na Kenya Kwanza.
Bw Musyoka alimlenga Mbunge wa Taveta John Bwire, ambaye alisema alimsaidia kushinda uchaguzi wa 2022 lakini sasa anafanya kazi kwa karibu na chama tawala cha UDA.
“Ninawashukuru viongozi wangu wa Wiper walioamua kutojiunga na Kenya Kwanza. Chama tawala kijue kuwa Wiper bado ni chama imara. Inasikitisha kumuona mbunge wangu wa Taveta John Bwire, ambaye nilimpigia kampeni, sasa akiwa msemaji wa UDA hapa,” alisema.