Habari

Uchaguzi wa 2027 utakuwa ghali zaidi katika historia ya Kenya

Na COLLINS OMULO August 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UCHAGUZI Mkuu wa 2027 unatarajiwa kuwa ghali zaidi katika historia ya Kenya, huku makadirio yakionyesha kuwa serikali, vyama vya kisiasa na wagombea watatumia zaidi ya Sh272 bilioni katika mchakato mzima wa uchaguzi.

Kiasi hicho kinajumuisha bajeti ya Sh74.8 bilioni ambayo Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imekadiria kwa ajili ya kuendesha uchaguzi huo pamoja na takriban Sh197.35 bilioni ambazo wagombea wanaweza kutumia katika kampeni zao iwapo watazingatia viwango vya matumizi vilivyowekwa na tume hiyo.

Kwa miaka mingi, uchaguzi nchini Kenya umejulikana kwa nyimbo, kauli mbiu na kampeni za kuvutia. Hata hivyo, matumizi makubwa ya fedha yameibua maswali kuhusu vipaumbele vya taifa wakati sekta muhimu kama afya, elimu na kilimo zinaendelea kukabiliwa na changamoto za ufadhili.

Kiasi cha Sh272 bilioni ni zaidi ya nusu ya fedha zilizotumiwa kuendesha kaunti zote 47 nchini katika mwaka wa kifedha uliomalizika Juni 2025, ambazo zilikuwa Sh470.7 bilioni.

Pia fedha hizo zinaweza kulipa kikamilifu madeni ambayo serikali za kaunti zinadaiwa ya zaidi ya Sh156 bilioni.

Kwa mtazamo mwingine, kiasi hicho ni kikubwa kuliko bajeti za baadhi ya sekta muhimu katika uchumi. Kwa mfano, sekta ya afya ilitengewa Sh177.2 bilioni, elimu ya juu Sh163.9 bilioni na elimu ya msingi Sh136.6 bilioni katika bajeti ya hivi karibuni ya serikali.

IEBC inasema gharama kubwa ya uchaguzi inatokana na teknolojia ya uchaguzi, vifaa vya kutambua wapigakura, mifumo ya kutuma matokeo, karatasi za kura zenye vipengele vya usalama pamoja na ongezeko la idadi ya wapigakura.

Tume hiyo inalenga kusajili wapigakura milioni 28.5 kufikia mwaka 2027, ikilinganishwa na milioni 22.1 waliopiga kura mwaka 2022.

Ongezeko hilo litahitaji vituo vya kupigia kura 55,393 kutoka vituo 46,229 vilivyotumika mwaka 2022.

Kwa upande wa wagombeaji, viwango vipya vya matumizi ya kampeni vinaonyesha kuwa kinyang’anyiro cha kisiasa kitahitaji fedha nyingi zaidi. Mgombea urais ataruhusiwa kutumia hadi Sh6.1 bilioni, kutoka Sh4.7 bilioni mwaka 2022.

Wagombeaji wa ugavana, useneta, ubunge na uwakilishi wa wanawake pia watatumia mabilioni ya fedha katika kampeni zao.

Mbunge wa Likuyani, Innocent Mugabe, anasema kiwango cha matumizi kilichowekwa na IEBC ni cha chini ikilinganisha na hali halisi ya kampeni.

“Nilitumia takriban Sh50 milioni mwaka 2022. Ukiwa na nia ya kushinda, lazima utumie fedha zaidi,” alisema.

Kwa mujibu wa IEBC, mipaka ya matumizi ya kampeni inalenga kuhakikisha uchaguzi unakuwa wa haki, uwazi na uwajibikaji, na kwamba matokeo ya uchaguzi yanaamuliwa na wapigakura badala ya nguvu ya fedha.

Hata hivyo, baadhi ya viongozi wamehoji jinsi sheria hizo zitakavyotekelezwa, wakisema bado Kenya ina mfumo mkubwa wa matumizi ya fedha taslimu ambao ni vigumu kufuatilia.

Iwapo makadirio ya sasa yatatimia, uchaguzi wa 2027 utaweka rekodi mpya kama uchaguzi wa gharama kubwa zaidi kuwahi kufanyika nchini Kenya.