Lugha, Fasihi na Elimu

Makosa yaliyozoeleka ya kutumia maneno ‘gonjeka’ na ‘sanasana’

Na HELLEN NJAGI August 31st, 2026 Kusoma ni dakika: 1

LUGHA ya Kiswahili kama zilivyo lugha nyingine ina aina mbalimbali za maneno.

Mojawapo wa aina hizo za maneno ni kitenzi. Kitenzi ni neno ambalo hutoa taarifa au ujumbe kuhusu jambo lililofanyika au litakalofanywa.

Kuna baadhi ya watu wanaowasiliana kwa Kiswahili wenye mazoea ya kuunda kitenzi ‘gonjeka’ kutokana na nomino mgonjwa.

Ingawa hakuna neno *gonjeka katika Kiswahili, ni kawaida kulipata katika mawasiliano watu wanapozugumzia mtu ambaye ana maradhi.

Aghalabu utakumbana na sentensi kama vile: *Rafiki yangu hakuenda shuleni jana kwa sababu aligonjeka. *Watoto hao waligonjeka baada ya kunywa maji machafu.

Ingawa ujumbe katika mifano hii ya sentensi unaeleweka,sentensi zenyenwe si sahihi. Ni kosa kusema mtu aligonjeka.

Ili kuzisahihisha sentensi ya kwanza tunafaa kusema: Rafiki yangu hakuenda shuleni jana kwa sababu alikuwa mgonjwa.

Vilevile, tunaweza kuisahihisha kwa kusema: Rafiki yangu hakuenda shuleni jana kwa sababu aliugua.

Sentensi ya pili itasahihishwa kwa kusema: Watoto hao waliugua baada ya kunywa maji machafu.

Pia kuna mazoea ya kuradidi kielezi sana na kuwa ‘sanasana’ ili kulitumia neno hilo katika sentensi kuleta maana ya kusisitiza ukweli.

Mara kwa mara utakutana na sentensi kama vile: *Wanafunzi wengi walifaulu katika tathmini ya taifa sanasana katika somo la Kiswahili. Si sahihi kusema sanasana.

Ili kuisahihisha sentensi hii tunafaa kusema: Wanafunzi wengi walifaulu katika tathmini ya taifa hasa katika somo la Kiswahili.

Pia tunaweza kuisahihisha kwa kusema: Wanafunzi wengi walifaulu katika tathmini ya taifa hususan katika somo la Kiswahili.