Habari za Kitaifa

Maraga atimiza vitisho, aanika ripoti ya polisi aliyompa Ruto

Na DANIEL OGETTA August 31st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JAJI Mkuu Mstaafu David Maraga ameonya kuwa Idara ya Polisi inayopendelea kisiasa inaweza kuingiza Kenya katika machafuko baada ya uchaguzi huku akimtaka Rais William Ruto kutekeleza kikamilifu Katiba.

Bw Maraga alisema hayo Jumatatu alipoweka wazi mapendekezo ya Jopokazi kuhusu Mageuzi ya Polisi aliloongoza mnamo 2023.

“Polisi wanaoegemea mrengo mmoja kisiasa ndio walikuwa kiini cha ghasia za 2007/2008. Wakenya hawapaswi kusahau kwamba vifungu vya Katiba ya 2010 kuhusu taasisi huru viliandikwa kwa damu hiyo,” akasema Bw Maraga.

Wiki iliyopita, Bw Maraga alimpa Rais Ruto makataa ya siku saba kuchapisha ripoti ya jopo kuhusu mageuzi ya polisi iliyowasilishwa kwake, akisema atachapisha mwenyewe iwapo serikali haitafanya hivyo.

SOMA PIA: Maraga ampa Ruto siku saba achapishe ripoti iliyopendekeza mageuzi ya polisi lau sivyo aitoe yeye

Alisema jopo lilipendekeza idara huru ya polisi ili kukomesha kile alichokiita kutekwa kwa Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) na kutumiwa vibaya kwa idara hiyo.

Hayo ni miongoni mwa mapendekezo zaidi ya 200 yaliyotolewa na kikosi hicho kulingana naye.

Bw Maraga ametaka mapendekezo hayo yote kutekelezwa, yakiwemo kuhakikisha uhuru wa NPS na kubadilisha sare za polisi.

Hata hivyo, alisema mabadiliko ya sare hayakuwa jambo la dharura. NPS ilizindua sare mpya wiki iliyopita.

Alisema Kenya sasa inashuhudia kile alichowahi kukiita “vurugu za kisiasa zilizopangwa, magenge na polisi wenye misimamo ya kisiasa”.

Alitoa mfano huo kutokana na ghasia zilizoshuhudiwa Homa Bay, Keumbu na Ol Kalou, pamoja na visa vya vurugu katika makanisa ya Kisumu, Nairobi na Witima.

Katika kisa cha Homa Bay, watu wawili, akiwemo polisi mmoja, waliuawa na wengine 46 kujeruhiwa katika mapigano yaliyovuruga mkutano wa Linda Mwananchi.

“Jibu la tatizo hili ni kutii Katiba na Huduma ya Kitaifa ya Polisi lazima iwe huru. Ni hitaji la kuvunja mfumo wa polisi wa kikoloni na kukomesha kutekwa kwa mfumo wa usalama na serikali,” akasema Bw Maraga.

Alisema ingawa Katiba iko wazi kuhusu uhuru wa polisi, Sheria ya Marekebisho ya Sheria za Usalama ya 2014 iliondoa kinga hizo na kusababisha NPS itekwe.

Jopo la Bw Maraga lilipendekeza kufutwa kwa marekebisho hayo ya 2014 lakini anadai mapendekezo hayo yalipuuzwa.

Alisema pia sheria kuhusu umri iligeuzwa na matokeo yake yakawa kwa faida ya wazi ya kisiasa.