Siasa

Sakaja na Aladwa pabaya Nairobi wabunge wa ODM wakianza kuunga Babu hadharani

Na CECIL ODONGO September 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

CHAMA cha ODM kinakabiliwa na kibarua kigumu katika kuamua mgombea wake wa ugavana Nairobi baada ya baadhi ya wabunge kujitokeza hadharani kumuunga mkono Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, anayehusishwa na mrengo wa Linda Mwananchi.

Hii ni licha ya mbunge wa Makadara George Aladwa, ambaye ni mwenyekiti wa ODM katika Kaunti ya Nairobi, kutangaza azma yake ya kuwania kiti hicho.

Gavana Johnson Sakaja naye anadaiwa anatathmini iwapo atawania ugavana kupitia ODM.

UDA na ODM zinapanga kushirikiana kisiasa, kugawana nafasi na kuimarisha ushawishi wao katika jiji kuu kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

Mwishoni mwa wiki, Seneta wa Homa Bay Moses Kajwang’ alitangaza hadharani kumuunga mkono Bw Owino, ambaye ametofautiana na uongozi wa ODM na anahusishwa na mrengo wa Linda Mwananchi unaoongozwa na Edwin Sifuna na James Orengo.

“Babu usifanye mzaha na Nairobi, ichukue Nairobi,” akasema Bw Kajwang’ akiwa Oyugis huku umati ukishangilia.

Seneta huyo alikuwa akizungumza wakati wa mazishi ya mwanawe mwanasiasa wa Kasipul, Newton Ogada. Bw Owino na Gavana Orengo pia walihudhuria.

Mbunge wa Awendo Walter Owino pia amemuunga mkono Bw Owino, akisema ndiye mtu anayefaa zaidi kuongoza jiji.

“Babu anataka kuwa gavana wa Nairobi na Waluo wote wa Nairobi wanapaswa kumuunga mkono. Baada ya kutathmini jinsi atakavyotekeleza majukumu hayo ndipo tunaweza kufikiria na kumpa nafasi yenye mamlaka zaidi,” akasema Bw Walter Owino katika mahojiano na kituo kimoja cha eneo hilo.

Mbunge wa Lang’ata Phelix Odiwour, almaarufu Jalang’o, pia amewahi kumuunga mkono Bw Owino, ambaye yuko katika muhula wake wa pili kama Mbunge wa Embakasi Mashariki.

“Ninajiandaa kwa uongozi wa Babu Owino kama gavana wa Nairobi. Najua anakuja kuhudumu kwa muhula mmoja, na baada ya hapo, atanipisha mimi huku yeye akipanda hadi nafasi ya juu zaidi,” akasema Bw Odiwuor.

“Ikiwa Babu Owino atapewa tiketi ya ODM, atakuwa gavana wa Nairobi. Asipopewa, atasababisha tabu kwa wagombea wengine,” akaongeza.

Huko Homa Bay, Bw Owino alishangaa kwa nini ODM inataka kumpa Bw Sakaja tiketi ya ugavana, ilhali hakuwahi kumuunga mkono aliyekuwa kiongozi wa ODM, marehemu Raila Odinga.

“Mimi ndiye gavana ajaye wa Kaunti ya Nairobi. ODM inataka kumpa Sakaja tiketi ilhali 2007 alimuunga mkono Kibaki, kisha 2013 na 2017 akamuunga mkono Uhuru kabla ya kumuunga mkono Ruto 2022. Hakumtaka Raila, lakini sasa anapendekezwa kuwania ugavana,” akasema Bw Owino.

Matarajio ya Bw Sakaja kujiunga na ODM pia yamezua wasiwasi kwa Bw Aladwa, ambaye amesisitiza kuwa uteuzi wa chama hicho unapaswa kuwa huru na wa haki.

“Nimeunga mkono na kukiimarisha chama hiki cha ODM kwa miaka mingi na kila mtu anajua kwamba tulifanya kazi kwa karibu na kiongozi wetu wa chama aliyefariki, Raila Odinga. Wale wanaopanga kujiunga na ODM wawe tayari kwa mchujo. Madiwani wote na wajumbe wako nyuma yangu,” alisema Bw Aladwa.

Kiongozi wa ODM Dkt Oburu Oginga aliwahi kusema chama hicho kinaweza kumuunga mkono Bw Owino iwapo watakuwa katika kambi moja ya kisiasa.

“Babu aliniambia kwamba analenga kura za Mlima Kenya na Wakamba, na kubaki ODM kutahatarisha nafasi zake. Hata hivyo, ninamhofia kwa sababu anaweza kupoteza kura zetu iwapo hatashirikiana nasi,” alisema Dkt Oginga mwezi Machi baada ya kukutana na Bw Owino.