Hivi Orengo na sifuna wameingia katika uga wa mapambano?
TANGAZO la Gavana wa Siaya, James Orengo, kwamba analenga kuwania urais wa Kenya mwaka 2027 kupitia vuguvugu la Linda Mwananchi linatibua donda jipya katika siasa za upinzani nchini.
Hatua hiyo inazua maswali mazito kuhusu mustakabali wa upinzani, urithi wa kisiasa wa Raila Odinga na hatima ya siasa za Nyanza baada ya kuondoka kwa mwanasiasa huyo aliyekuwa mhimili wa eneo hilo kwa miongo kadhaa.
Si mara ya kwanza Orengo anaonekana kuwa na msimamo tofauti na wanasiasa wengine katika chama.
Historia yake na Raila ni ya ushirikiano uliochanganyika na ushindani wa kisiasa na tofauti za kimtazamo.
Orengo si mgeni katika siasa za urais; aliwahi kuwania kiti hicho mwaka 2002, wakati Raila naye alikuwa akijenga ushawishi wake katika siasa za kitaifa kisha kushirikiana naye tena katika serikali pana.
Kwa mtazamo wa kisiasa, ushirikiano huo haupaswi kutafsiriwa kama kutoweka kwa tofauti zao za kimkakati.
Orengo alilazimika kufanya kazi ndani ya mfumo ambao tayari ulikuwa na kiongozi mwenye mamlaka makubwa ya kisiasa kumzidi baada ya kivuli cha Raila kumfunika na kumzidi uwezo.
Orengo huenda aliona kuwa ushindani wa moja kwa moja dhidi ya Raila ungeweza kupunguza nafasi yake ya kisiasa.
Pengo la kuondoka kwake Raila limempa ujasiri wa kuibuka na sasa anaonekana kutaka kuwa mmoja wa wahusika wakuu katika mapambano hayo.
Kujikita kwake katika Nyanza kupitia Linda Mwananchi kunaweza kutafsiriwa kama mkakati wa kujenga kituo kipya cha mamlaka ambacho kinaweza kushindana moja kwa moja na ODM na uongozi wake wa sasa.
Katika hatua za awali za Linda Mwananchi, Orengo alionekana kumuunga mkono Edwin Sifuna katika matarajio yake ya kuwania urais.
Sifuna amekuwa akijijenga kama sura mpya ya kisiasa yenye uwezo wa kuvuka mipaka ya ODM na kuunganisha kizazi kipya cha wapiga kura.
Sasa Orengo anabadili rangi na kuvalia ngozi ya mgombea wa urais chini ya mwavuli huo huo. Je, Orengo amebadilisha wazo lake, au ameingia katika mradi wa Sifuna akiwa na njama tofauti ya baadaye?
Kwa wafuasi wa Sifuna, hii inaweza kuonekana kama usaliti wa kisiasa.
Kwa upande wa Orengo, inaweza kutetewa kama haki yake ya kushiriki katika kinyang’anyiro cha kuwania uongozi wa nchi.
Changamoto kubwa sasa ni iwapo Linda Mwananchi inaweza kubeba matarajio mawili ya urais bila kugawanyika.
Ikiwa Orengo na Sifuna watashindwa kufikia makubaliano kuhusu uongozi, vuguvugu hilo linaweza kugeuka kutoka chombo cha kuunganisha upinzani na kuwa uwanja wa mapambano ya madaraka.
Kwa Orengo tajriba yake ya kisiasa na ujasiri wa kupambana dhidi ya mababe wa kisiasa sharti itazamwe kwa jicho la pili.
Hii ni fursa yake kujijenga kama mrithi wa nafasi ya kisiasa iliyoachwa wazi na Raila. Lakini pia ni kamari kubwa.
Hesabu zake Orengo kogombea kiti cha urais zinaweza kutia pilipili katika macho ya Sifuna na viongozi wenza katika ndoto ya kuwania urais.
Pambano kuelekea 2027 halitakuwa tu upinzani dhidi ya rais Ruto.
Itakuwa pia vita vya ni nani atadhibiti urithi wa Raila, ni nani atamiliki Nyanza kisiasa, na nani atakuwa uso mpya wa upinzani nchini Kenya.