• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:55 AM
MAWAIDHA YA KIISLAMU: Chumo haramu ni miongoni mwa dhambi za kutupeleka jehanamu

MAWAIDHA YA KIISLAMU: Chumo haramu ni miongoni mwa dhambi za kutupeleka jehanamu

Na HAWA ALI

SIFA zote njema anastahiki Mungu Azzawajalla, swala na salamu zimwendee Mtume Mtukufu Swallallahu A’alayhi Wasallam.

Amesema Allah Subhanahu wataala “Hakika mali zenu na watoto wenu ni fitna” (Taghaabun 15).

Mali ni fitna kwani ni kama upanga wenye ncha mbili, ambao ima itamnufaisha mtu au kumuangamiza; ima aichume katika njia za halali imnufaishe duniani na akhera, au aichume kwa njia haramu imnufaishe duniani na kumuangamiza akhera, Mtume rehema na amani ziwe juu yake ametuambia kuwa kila mtu ataulizwa mambo manne siku ya kiama na akataja kuwa moja ni mali; vipi kaichuma na vipi kaitumia, hivyo mali itakuwa na maswali mawili tofauti na mambo mengine yenye swali moja kwa kila jambo.

Uislamu haukatazi mtu kuwa na mali nyingi almuradi kachuma katika njia za halali na anazitumia zinavyostahiki, kwani historia imewataja baadhi ya waja wema waliokuwa matajiri na namna gani walivyozitumia mali zao katika kumridhisha Mola wao; tukianzia maswahaba akina Sayyidina Uthmaan, Abdul-Rahmaan bin Auf na maswahaba wengineo na wema waliokuja baada ya hapo radhiallahu anhum ajmain.

Amesema Mtume rehma na amani ziwe juu yake: “Ni mali bora iliyoje iliyokuwa nzuri inayomilikiwa na mtu mzuri” inaonesha kuwa mtu mwema anapomiliki mali basi hata mali yake huwa nzuri kwani hutolewa na kutumiwa katika njia anazozipenda Allah subhaanah.

Lakini pia Uislamu umekataza kuchuma mali kwa njia za haramu. Umekataza kuchuma mali kwa mambo aliyoyaharamisha Allah subhaanahu wataala: Tunaona tamaa za watu za kutaka kutajirika kwa haraka, wanatumia njia ambazo Allah ameharamisha, toka asili ya kile kitu seuze biashara yake. Na tutazame mifano michache:

Mifano

Allah subhanahu wataala amekataza ULEVI, hivyo hata biashara yake haifai. Tunaona katika hadithi ya Mtume Rehma na amani ziwe juu yake watu kumi wanaohusu ulevi wamelaaniwa. Toka muuzaji mpaka mkokoteni uliobeba pombe pia umelaaniwa. Ni vijana wangapi tunaoishi nao washalaaniwa? Vijana wangapi walojazana katika mahoteli kunakouzwa pombe na wao kushiriki katika biashara hiyo?
Vile vile, Allah subhanahu wataala amekataza RIBA, lakini tunaona inavyochotwa katika benki na kwingineko mpaka kupambiwa majina ili ionekane kuwa ni halali. Tumeona kuwa kilichoharamishwa na sheria ni haramu na riba ni haramu. Katika kitabu na Sunnah, amesema Allah “Na Allah amehalalisha biashara na kuharamisha riba” Baqarah 275, na kuna hadithi nyingi zinazoonesha ukubwa wa dhambi ya riba ikiwemo riba kuwa miongoni mwa madhambi saba yenye kuangamiza na ile hadithi ya Mtume kuwa riba ina milango 70; wa chini yao ni mfano wa mtu kuzini na mamake.

Aidha, tumekatazwa kula RUSHWA. Tunaona suala la rushwa liko kila kona, si wanasiasa tu wanaokemea rushwa, Uislamu umetangulia kuikemea rushwa na kuonesha kuwa Mtoaji, mpokeaji na anaeshuhudia wote wamelaaniwa. Imekuwa haki yako huipati mpaka utoe rushwa yaani laana za Allah zimejaa kila kona kiasi cha kutukosesha barka katika miji yetu.

Pia Allah subhanahu wataala amekataza kula MALI YA YATIMA. Hata hivyo ni wangapi wanafikia hata kiasi cha kupora haswaa mali za mayatima, wakisahau maneno ya Allah aliposema: “Hakika ya wale wanaokula mali ya mayatima kwa dhulma hakika wanakula moto katika matumbo yao…” (Nisai 10). Tayari washatia moto katika matumbo yao toka duniani kabla ya kufika Akhera. (Allah atuhifadhi).

Allah subhanahu wataala pia amekataza MUZIKI, hivyo biashara yake pia ni haramu kama alivyosema Mtume rehema na amani ziwe juu yake; kuwa biashara yake haina faida, wala thamani, lakini ni vijana wangapi wanashiriki kutoa, kuuza na kusambaza CD na mengineyo yanayohusu muziki?

Allah subhanahu wataala vilevile amekataza UZINIFU; hivyo kila kinachohusu na kuchangia uzinifu ni haramu, kwani tumekatazwa hata kuikaribia zinaa. Lakini ni watu wangapi wanafanya kazi kwenye sehemu zenye kuchochea zinaa au kushiriki katika uuzaji wa vitu vyenye kuchochea uzinifu? Haya yote ni haramu na mwenye kusaidia kufanya jambo baya basi na yeye atapata malipo sawa na mfanyaji pasi na kupunguziwa chochote.

Allah subhanahu wataala aidha amekataza SHIRKI. Ni vijana wangapi wanatafuta utajiri kwa njia za kishirikina na kufikia sasa wanawaua wenzao kwa sababu ya mali? Ni haramu juu ya haramu. Tutaenda kumjibu nini Allah subhanahu wataala atakapotuuliza kuhusu mali; namna tulivyoichuma na kuitumia? Mifano ya njia za haramu iko mingi ambayo imeenea katika jamii.
Tunaona migogoro ya ardhi na watu kupora ardhi si zao, na baadaye kudai ni zao ili waziuze wanufaike! Ni makosa mtu kuzidisha shubiri moja tu ya ardhi isiyo yake seuze kupora ardhi.

Ndugu zangu wa Kiislamu, Mtume ametuonya pale aliposema katika hadithi ya Abdullah bin Mas-uud na kupokewa na Bukhari na Imam Ahmad rahimahumallah “Hatochuma mja mali ya haramu kisha akaitoa (kwa kuitumia) Allah akambarikia, wala hatoitolea sadaka Allah akamkubalia, wala hatoiwacha nyuma yake (baada ya kufa) isipokuwa itakuwa ni akiba yake ya kumpeleka motoni. Subhnallah!

Mali ya haramu haina manufaa yoyote si katika kuitumia kulisha familia au kujilisha mtu mwenyewe, wala si katika kuitolea sadaka, na ukiiacha pia ni mashaka. Allah atuhifadhi.

You can share this post!

UKUMBI WA LUGHA NA FASIHI: Utahini wa Karatasi ya Kwanza...

Reds wazuru St Marys jicho likiwa kileleni

adminleo