• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 11:28 AM
SHANGAZI: Nilimfumania ndani ya gari akigawa asali. Nitafanya nini?

SHANGAZI: Nilimfumania ndani ya gari akigawa asali. Nitafanya nini?

Na SHANGAZI SIZARINA

Pokea salamu zangu shangazi. Ninaumwa sana moyoni baada ya mwanamke mpenzi wangu kusaliti penzi letu. Juzi mimi naye tuliandamana na mwanaume rafiki yangu katika maskani fulani ya starehe. Tuliburudika kwa vinywaji na wakati fulani wawili hao wakatoka kila mmoja akisema anaenda msalani. Walipokawia nilitoka kuwatafuta na nikawafumania ndani ya gari la rafiki yangu. Baadaye mpenzi wangu aliniomba msamaha akidai alikuwa amelewa na hakujua alichokuwa akifanya. Ninampenda sana na sijui nitafanya nini.
Kupitia SMS

Kuna usemi kuwa kikulacho ki nguoni mwako. Sasa umejua kuwa mwanamume huyo unayemuita rafiki yako si rafiki hasa bali ni mbwa mwitu ndani ya ngozi ya kondoo. Sidhani unaweza kumwamini tena kwa hivyo itabidi uvunje urafiki huo. Huenda mpenzi wako pia alikuhadaa eti alikuwa mlevi, lakini unaweza kumpa nafasi nyingine kisha uendelee kuchunguza kwa makini mienendo yake.

 

Nilipata mchumba akiwa na wake wa zamani

Vipi shangazi. Nimechumbia mwanamke fulani na tunaendelea kupanga harusi. Hata hivyo nilishangaa sana juzi nilipomtembelea nyumbani kwake kama kawaida na nikampta na mwanaume aliyekuwa mpenzi wake. Sijamuuliza walikuwa wakizungumzia nini lakini nina wasiwasi. Nishauri.
Kupitia SMS

Bila shaka ni lazima uwe na wasiwasi hasa ukizingatia kwamba wawili hao walikuwa wapenzi. Isitoshe, mwanaume huyo amemtembelea wakati ambao mnaendelea na mipango yenu ya harusi. Badala ya kunyamaza na kuumia kwa hofu, ni muhimu umuulize mpenzi wako ili ujue kiini hasa cha mpenzi wake wa zamani kumtembelea.

 

Ananikataza kulima shamba

Vipi shangazi? Kuna mwanamke ambaye tumekuwa na uhusiano kwa mwaka mmoja sasa na nampenda sana. Tatizo ni kuwa nikitaka penzi lake yeye hunipa vijisababu vya kila aina. Amenishinda, tafadhali nishauri.
Kupitia SMS

Kila kitendo kina sababu. Labda mwananke huyo hakupendi ama anahisi kwamba unamharakisha sana. Kumbuka mmejuana kwa mwaka mmoja pekee na huenda anahitaji muda zaidi ili akujue vizuri. Kuwa na subira kwani mvumilivu hula mbivu.

 

Aliaga nikiwa mjamzito

Habari yako shangazi. Nina umri wa miaka 21 na ninaishi maisha ya kujuta. Sababu ni kuwa nilipata mtoto nikiwa mchanga baada ya kudanganywa na mwanamume fulani. Aliaga dunia nikiwa na mimba ya mtoto huyo na kuniachia mzigo wa kumlea. Natafuta mwanamume ambaye atanioa pamoja na mtoto wangu na amkubali kama wake. Tafadhali nisaidie.
Kupitia SMS

Tunaambiwa kuwa majuto ni mjukuu, huja kinyume. Kadhalika, maji yaliyomwagika, hayawezi kuzoleka. Ninaamini ujumbe wako huu utawafikia wanamume wanaotafuta wake na labda kuna atakayevutiwa akitafute. Nakutakia kila la heri.

 

Amekosa uaminifu
Kwako shangazi. Kuna kijana fulani ambaye amekuwa akiniambia eti ananipenda lakini juzi nilishtuka nilipomfumania na msichana mwingine. Baadaye alinitumia ujumbe wa SMS akiomba nimsamehe na kusisitiza kuwa ni mimi tu anayependa. Tafadhali nishauri.
Kupitia SMS

Hata kama unafikiria kumsamehe, ni muhimu kwanza ujue iwapo kuna chochote kinachoendelea kati yake na msichana uliyewapata pamoja. Ni baada ya hapo ambapo utaweza kufanya uamuzi wa busara.

 

Amedai kuonja asali, nipakue?
Kuna mwanaume ambaye tumekuwa na uhusiano kwa miezi kadhaa na tumekutana mara tano tangu tujuane. Amenialika kwake na ameniambia wazi kuwa anataka asali. Je, niende ama nisiende?
Kupitia SMS

Umejua kwa hakika kwamba mwaliko wa mwanaume huyo kwake ni wa kuonja asali. Kwa sababu hiyo, ukienda atajua kwamba umempelekea asali na ukikataa hatakuelewa. Kama huko tayari kumpakulia, basi usiende. Kutana naye mahali tofauti umwelezee sababu.

 

You can share this post!

TAHARIRI: Haki itendewe wote Turkana

Uhuru ategwa na wanyakuzi wa ardhi

adminleo