• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Maandamano dhidi ya Gavana Sang yatibuka

Maandamano dhidi ya Gavana Sang yatibuka

Na TOM MATOKE

MAANDAMANO yaliyopangwa kufanyika Ijumaa dhidi ya seneta wa Nandi, Stephen Sang yalitibuka dakika ya mwisho baada ya mmoja wa waandalizi kutoweka na kibali cha polisi na vifaa vilivyopaswa kutumiwa katika shughuli hiyo.

Bw Shadrack Kemei ambaye alikuwa na leseni hiyo na vifaa vingine kama firimbi na mabango hakuweza kupatikana Ijumaa asubuhi.

Baadhi ya waandamanaji waliwasili mjini Kapsabet saa kumi na mbili asubuhi na kusubiri viongozi wao kwa saa kadhaa ili waanze maandamano dhidi ya Gavana Sang.

Hata hivyo, walitawanyika mwendo wa saa sita adhuhuri walipokosa kumpata Bw Kemei na kuapa kwamba watapanga siku nyingine ya kufanya maandamano.

Maandamano hayo yaliitishwa na Seneta wa Kaunti ya Nandi Samson Cherargei na mwenyekiti wa chama cha Jubilee katika kaunti hiyo Sammy Biwott kulalamikia madai ya ufisadi katika serikali ya Gavana Sang.

Ijumaa, Bw Biwott alisema hawakuweza kumpata Bw Kemei au kupata vifaa walivyonuia kutumia kwenye maandamano.

Alisema waliahirisha maandamano hadi siku nyingine na kwamba hawatamwamini mtu mmoja kuwawekea vifaa hivyo.

“Watu wa Nandi walimchagua Gavana Sang kwenye uchaguzi mkuu wa 2017 alipoahidi kubadilisha kaunti yao na kuleta mageuzi lakini ufisadi umeongezeka tangu alipoingia ofisini,” alidai Bw Biwott.

Kulikuwa na maafisa wengi wa polisi mjini kabla ya maandamano hayo kufutiliwa mbali.

You can share this post!

NASAHA ZA RAMADHAN: Chakula cha daku humpa nguvu mfungaji...

Magoha aonya Knut vikali kwa kupinga mtaala mpya

adminleo