• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
Mwekezaji ataka Joho atupwe jela miezi 6

Mwekezaji ataka Joho atupwe jela miezi 6

PHILIP MUYANGA Na CHARLES LWANGA

MFANYABIASHARA aliyeshtaki serikali ya Kaunti ya Mombasa kufuatia mzozo wa shamba, sasa anataka Gavana Hassan Ali Joho aadhibiwe kwa kukaidi agizo la mahakama.

Bw Ashok Doshi na mkewe Pratibha, wanataka Gavana Joho, afisa mkuu wa idara ya ardhi Jaffer Mohesh na diwani Benard Ogutu wafungwe miezi sita gerezani kwa kupuuza agizo la mahakama.

Kupitia kwa wakili wao Willis Oluga, Bw Doshi na mkewe wanasema kuwa mahakama ilitoa agizo la kupiga marufuku serikali ya kaunti kubomoa ukuta, jengo au kuharibu mali yoyote iliyoko katika kipande chake cha ardhi.

Mlalamishi anasema kuwa mnamo Mei 10 mwaka huu, maafisa wa serikali ya kaunti wakiongozwa na Bw Joho pamoja wanasiasa wengine kutoka Mombasa, wallikodisha wahuni ambao walivamia shamba lake na kubomoa lango huku wakimshutumu kwa madai kuwa ni mnyakuzi wa ardhi.

“Gavana wa Mombasa alifanya mkutano wa kisiasa ndani ya shamba hilo akidai kwamba yeye ndiye ‘rais’ wa kaunti, na kisha akabatilisha hatimiliki ya ardhi hiyo,” anasema mlalamishi katika stakabadhi zake kortini.

Mlalamishi anasema Bw Joho, Bw Mohesh na na diwani Bw Ogutu walikaidi agizo la mahakama kwa kuvamia ardhi hiyo na kumtatiza kuitumia.

Mlalamishi anasema kuwa Gavana Joho na Bw Ogutu, wakiwa watumishi wa umma, wanafaa kuwa kielelezo bora kwa kuheshimu korti na kudumisha amani badala ya kutumia wahuni kuzua rabsha.

Kwingineko, Hakimu Mkuu katika mahakama ya Malindi, Bi Julie Oseko jana alimshtumu Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) Nordin Haji, kwa kuchelewa kuwasilisha mashahidi kwenye kesi.

Bi Oseko alisema upande wa mashtaka umewasilisha mashahidi wanne pekee katika kesi ambapo mwanamke na afisa wa polisi wameshtakiwa kwa kuhujumu kesi.

“Kwa nini mashahidi wanne pekee watoe ushahidi katika kipindi cha miaka miwili tangu kesi ianze? ” akasema Bi Oseko.

Alizungumza baada ya kusikizwa kwa kesi ambapo Bi Amina Shiraz pamoja na Sajenti Abdi Sheikh wameshtakiwa kwa kuficha ushahidi wa mauaji ya Bw Jimmy Baburam anayedaiwa kuuawa na mkewe, Bi Shiraz katika hoteli ya Medina Palms eneo la Watamu, mnamo Julai 26, 2015.

Wakati wa kesi kusikizwa, aliyekuwa kamanda wa polisi Watamu, Bw Michael Ndonga alisema kuwa daktari aliyekuwa anashika doria katika hospitali ya Watamu Nursing Home alimwabia kuwa Bw Baburam alikuwa ameshaaga dunia wakati alifikishwa katika hospitali hiyo.

“Nilipofika katika hospitali ambapo marehemu alipelekwa, niliangalia na nikaona kuwa mwili huo haukuwa na alama yoyote ya kuumizwa,” alisema.

Bw Ndonga alisema alienda katika hoteli ya Medina Palms kulitokana baada ya mkuu wa usalama katika hoteli hiyo kumpigia simu ya kuwa mtalii mwanaume amefariki chumbani mwake.

“Aliniambia kwa simu kuwa mtalii aliyekuwa ameabiri chumba mnamo Julai 21, 2015 hadi Julai 27, 2015 amefariki chumbani na alikuwa anataka niende nikaone mahali alifariki,” alisema.

Bw Ndonga ambaye sasa hizi ni Naibu Kamada wa polisi Kaunti Ndogo ya Voi, alisema kuwa aliambatana na polisi mwenzake, Konstebo Mutua hotelini na wakapata damu sakafuni, chupa za pombe, taulo na chupa za kunywea pombe kando ya dimbwi la kuogelea.

Alisema kuwa baada ya hapo walielekea hospitalini ambapo mwili huo unadaiwa kupelekwa na wakampata mwamerika anayesakwa na polisi pamoja na Bi Shiraz akiwa analia.

“Bi Shiraz alikuwa ameambatana na mwanaume ambaye alijitambulisha kama Bw Jacob Schmalze na akasema kuwa yeye ni rafiki wa familia ya marehemu,” alisema.

Bali na shtaka la kunyimana haki, Bi Shiraz pamoja na raia huyo wa Amerika wanakabiliana na shtaka lengine katika Mahakama ya Mombasa ya kumuua Bw Baburam.

Kesi inaendelea kusikizwa.

 

You can share this post!

Mvua yazua maafa Pwani

Nikishindwa 2022 nitajiunga na upinzani – Ruto

adminleo