• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 3:03 PM
Rais aonywa dhidi ya kuzamisha jahazi la Jubilee

Rais aonywa dhidi ya kuzamisha jahazi la Jubilee

Na MWANGI MUIRURI

RAIS Uhuru Kenyatta sasa ameonywa na baadhi ya wandani wake kisiasa kuwa anahatarisha chama cha Jubilee kuzama kisiasa na kijipate kikiwa hafifu kuwania urais 2022.

Ameonywa kuwa katika siku za hivi majuzi amegeuka kuwa dikteta wa kimaamuzi na ambaye hatii mpangilio wa demokrasia ya vyama vya kisiasa ambapo amegeuza taifa kuwa lisilo na chama chochote cha kisiasa.

Ameambiwa kuwa sera yake ya kukumbatia upinzani ndani ya serikali hata ikiwa ni ya busara katika kusaka umoja na amani ya nchi, vigezo vya demokrasia ya kudumu lazima kiwe ni kuweko kwa vyama vya kisiasa vilivyo thabiti.

Mbunge wa Kapseret, Oscar Kipchumba Sudi katika mtambo wake wa Twitter ameonya kuwa rais Kenyatta amegeuza chama cha Jubilee kuwa mali yake binafsi na ambapo hatambui vyombo vya kufanya maamuzi.

“Wakati mmoja amegeuka kuwa msemaji, mratibu, mkosoaji, kiongozi wa mashtaka, basi hiyo si demokrasia iliyo wazi, ni udikteta,” akasema.

Aidha, Bw Sudi alilia kuwa Jumapili iliyopita Rais alitangaza kuwa sio wanasiasa waliochaguliwa katika uchaguzi mkuu wa Jubilee ambao walimpa ushindi wa urais.

“Sio wao walinifanya kuwa rais…mimi ndiye niliwatafutia kura na wakawa vile walivyo…Wanacheza na mimi…mimi nitawatoa kwenye wako sasa, ngoja utaona,” akafoka rais akiwa katika kongamano na imani ya Wakorino katika ukumbi wa Kasarani, Nairobi.

Sasa, Sudi anaonya rais Kenyatta kuwa “kuna wengi ambao walijitolea kufa kupona kumpigia debe kwa wapiga kura kiasi kwamba hata wengine walipoteza utajiri na mali katika harakati hizo.”

 

You can share this post!

Chokoraa waelezea hofu yao kaunti ikianza kuwasajili

Aibu kizimbani mwanamume kubaka nyanyake wa miaka 90

adminleo