• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 9:50 AM
Raila asifu Sapit kwa kupigana na ufisadi kanisani

Raila asifu Sapit kwa kupigana na ufisadi kanisani

Na RUSHDIE OUDIA

KIONGOZI wa ODM Raila Odinga amemiminia sifa Kiongozi wa Kanisa la Anglikana (ACK) Jackson Ole Sapit kwa kupiga marufuku michango ya fedha kutoka kwa wanasiasa.

Bw Odinga alisema hatua ya Askofu Mkuu Sapit inasaidia katika kukabiliana na ufisadi ambao umekolea nchini.

Kumekuwa na mjadala kuhusiana na mamilioni ya fedha yanayotolewa na wanasiasa makanisani huku Bw Odinga na Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) Noordin Hajji wakiamini kuwa michango hiyo inaendeleza wizi wa fedha za walipa ushuru.

Bw Odinga alidai kuwa wanasiasa wa kundi la Tangatanga linalounga mkono Naibu wa Rais William Ruto linatumia fedha kujitafutia umaarufu nchini.

Bw Odinga alikuwa akizungumza katika Kaunti ya Siaya wakati wa hafla ya kusherekea kustaafu kwa Askofu wa Parokia ya Maseno Magharibi Dkt Joseph Otieno Wesonga.

Alisema uchumi wa Kenya umedorora kutokana na ufisadi.

“Wanasiasa sasa wanawahonga viongozi wa kidini ili wawaalike kanisani kufanya mchango. Fedha hizo zinatokana na ufisadi na wanazitumia kununua watu wa kuwaunga mkono,” Bw Odinga.

“Hata wafanyabiashara maarufu kama vile Vimal Shah na Manu Chandaria ambao wamekuwa wakisaidia jamii hawawezi kutoa mamilioni ya fedha kila wikendi,” akasema.

Suala kuhusu harambee kanisani limekuwa likiibua mjadala mkali, lakini Dkt Ruto husisitiza ataendelea kutoa michango hiyo kwa kuwa ni shukrani yake kwa Mungu.

You can share this post!

Serikali kukagua wanaume kubaini ikiwa wametahiriwa

Mkenya atupwa ndani maisha China kwa kulangua kokeini

adminleo