• Nairobi
  • Last Updated March 18th, 2024 8:55 PM
MAKALA MAALUM: Siasa za kuviziana zadhihirika katika uteuzi wa Uhuru kwenye Mahakama ya Rufaa

MAKALA MAALUM: Siasa za kuviziana zadhihirika katika uteuzi wa Uhuru kwenye Mahakama ya Rufaa

JAJI Paul Kihara Kariuki aliyeteuliwa na Rais Kenyatta kuwa Mwanasheria Mkuu. Picha/ Maktaba

Na RICHARD MUNGUTI

KINYANG’ANYIRO cha kuteua rais wa mahakama ya rufaa na mwakilishi wake katika tume ya Idara ya Mahakama (JSC) kilitifua vumbi kali wiki chache zilizopita, huku komeo za kudhibiti idara ya mahakama zikikosa kushikilia kama ilivyotarajiwa.

Siasa za kuviziana zilielekezwa katika mahakama hiyo ya pili kwa ukubwa nchini baada ya ile ya Juu na wadau wenye ushawishi mkubwa katika chama tawala cha Jubilee, lakini kura zilipopigwa, dau lao lilienda mrama.

Wale ambao hawakutarajiwa kushinda ndio walitwaa ushindi na sasa mahakama hiyo na JSC itafanyakazi na walioteuliwa.
Mahakama hiyo inayotarajiwa kuwa na majaji 30, kwa sasa ina majaji 18 baada ya baadhi yao kustaafu na wengine hawajateuliwa.

Kuna nyadhifa 12 katika mahakama hiyo kufuatia kuondoka kwa Jaji Paul Kihara Kariuki na kuwa Mwanasheria Mkuu.
Waliotazamiwa kutwaa nyadhifa hizo mbili zenye ushawishi mkubwa walilambishwa sakafu, na ndoto ya waliowatumainia kuwa na usemi katika Mahakama ya Juu kuambulia patupu.

Ushindani mkali ulizuka kujaza nafasi ya Jaji Kariuki alipoteuliwa na Rais Uhuru Kenyatta katika wadhifa wa Mwanasheria Mkuu baada ya Prof Githu Muigai kujiuzulu.

 

Kivumbi
Nyavu za kuwavua rais na mwakilishi katika JSC wa Mahakama ya Rufaa zilitandazwa na kampeni zikaanza kushika kasi.
Kilele kilikuwa wiki iliyopita wakati kura zilipopigwa na kivumbi kikatulia.

Waliomenyana kutwaa urais walikuwa Majaji Alnashir Visram, William Ouko na Martha Koome.

Watatu hao walifanya kila juhudi kuridhisha wenzao kuwateua, lakini Jaji Koome aliyekuwa anatazamiwa kushinda alijiondoa na kuwaacha Majaji Visram na Ouko wapimane nguvu.

Baada ya kura kupigwa, Jaji Ouko alimshinda Jaji Visram kwa kupata kura 16 kati ya kura zilizopigwa naye Jaji Visram akapata kura nne. Sasa Jaji Ouko ndiye rais wa Mahakama ya rufaa. Ametwaa wadhifa uliokuwa umeshikiliwa na Jaji Kariuki kwa miaka kadhaa.

Uteuzi wa Jaji Kariuki kuwa Mwanashera Mkuu utajadiliwa na kamati ya bunge inayohusika na masuala ya haki, upelekwe bungeni kuidhinishwa kisha jina lipelekwe kwa Rais Kenyatta.

Kamati ya bunge ya masuala ya haki inayoongozwa na Mbunge wa Baringo Kaskazini, Bw William Cheptumo itajidili suala hili la Jaji Kariuki na kupokea maombi  kutoka umma.

Katika kinyang’anyiro cha kumteua mwakilishi wa JSC, Jaji Mohammed Warsame alimshinda Jaji Wanjiku Karanja kwa kuzoa kura 16 kwa 4 na kupata kipindi kingine katika JSC.

Matokeo hayo ya kura yalituliza siasa za pembeni za Jubilee ambapo baadhi ya wanasiasa waliona idara ya mahakama kuwa iliyo na majaji wengi walioegemea mrengo wa Nasa.

Ili kutaka kudhibiti JSC, wanasiasa hao walimshauri Rais Kenyatta kuteua aliyekuwa Msimamizi wa Chuo Kikuu cha Kenyatta (KU) Profesa Olive Mugenda, aliyekuwa Waziri wa Kilimo Felix Koskei na aliyekuwa karani katika bunge la kitaifa Patrick Gichohi kuwa wanachama wa tume hii ya kuwaajiri majaji na mahakimu (JSC) ndipo Jubilee iwe na usemi mkuu katika idara ya mahakama.

Lakini uteuzi wao ulipigwa breki Kituo cha Katiba Institute kilipowasilishwa kesi kortini na maagizo yakatolewa yakisitisha kuapishwa kwa watatu hao (Mugenda, Koskei na Gichohi) hadi kesi iamuliwe.

 

Sheria ilikiukwa

Mamlaka ya Rais Kenyatta ya kuwateua watatu yanahojiwa katika kesi hii kwani Katiba Institute inadai sheria ilikiukwa.

Nafasi nyingine katika JSC ilitokea baada ya Rais Kenyatta kumteua Bi Winnie Guchu kuwa naibu ajenti mkuu wa kampeni na uchaguzi wake Agosti na Oktoba 2017 ambaye alimteua kuwa  Waziri msaidizi.

Kuchaguliwa kwa Jaji Ouko, kutoingia kwa Jaji Karanja na kutoapishwa kwa wateule watatu katika JSC kumepunguza kasi ya Jubilee kuthibiti mahakama ya rufaa na JSC.

Sasa ni wazi historia itajirudia katika uteuzi AG kwa vile nyakati za utawala wa rais mstaafu Daniel arap Moi aliyekuwa wakati mmoja Jaji wa Mahakama ya Rufaa marehemu Mathew Guy Muli alimteua kuwa mwanasheria mkuu.

Na baadaye Jaji Muli akastaafu kama Mwanasheria Mkuu na kuteuliwa tena kuwa Jaji wa Mahakama ya rufaa wadhifa aliohudumu hadi akahitimu miaka 74 na kustaafu. Jaji Muli alifungua afisi ya uwakili na alikuwa akihudumu kama wakili wa kibinafsi hadi alipopungia dunia mkono wa buriani.

Kuteuliwa kwa Jaji Kariuki kutakuwa ni kama kuhamisha huduma zake hadi kwa afisi ya AG ambayo katiba inasema anayeteuliwa kuutekeleza lazima awe amehitimu kuteuliwa kuwa jaji katika mahakama ya rufaa.

“Kwa mujibu wa mamlaka niliyopewa na Kifungu 156(2) cha Katiba nimemteua Jaji Kariuki kuwa Mwanasheria mkuu mpya wa nchi hii. Nimepeleka jina lake kwa bunge la kitaifa kuidhinishwa,” alisema Rais Kenyatta alipomteua.

 

Haijabainika

Wakati tangazo hilo lilipopeperushwa hakuna chochote kilisemwa iwapo Jaji Kariuki amejiuzulu na kufikia sasa haijabainika ikiwa amejiuzulu au la kwani JSC haijatoa habari.

Hiki ni kinyume na ilivyokuwa aliyekuwa mkurugenzi wa mashtaka ya umma (DPP) Keriako Tobiko alipong’atuka afisini.

Bw Tobiko alijiuzulu kisha Rais Kenyatta akatangaza amekubali kujiuzulu kwake kisha akamteua kuwa Waziri wa Misitu. Sivyo hivyo kwa Jaji Kariuki.

Kabla ya kuteuliwa kuwa jaji, Jaji Ouko alikuwa Msajili wa Idara ya Mahakama na kutokana kazi yake alikuwa akitangamana na majaji na mahakimu wote.

Alikuwa akihusika na maslahi yao ya kila siku na hivyo basi kipindi chake kama rais hakitakuwa na ugumu kutokana majukumu yake alipokuwa msajili.

Kazi ya rais wa mahakama ya rufaa ni kushughulikia masuala ya usimamizi na uteuzi wa majaji wanaosikiza rufaa mbalimbali. Pia huwa anafanya mikutano na Jaji Mkuu kuhusu korti hiyo.

 

Msimamo mkali

Duru zasema Jaji Warsame alishinda kuwa mwakilishi wa mahakama hiyo katika JSC kutokana na msimamo wake thabiti wakutopendelea upande wowote.

Msimamo wake mkali ulidhihirika alipokuwa akihudumu kama Jaji wa Mahakama kuu.

Wakati mmoja akiamua kesi aliwahi kumlaumu rais mstaafu Mwai Kibaki kwa kutotekeleza majukumu yake ya kikatiba ya kutia saini vibali vya kuwanyonga wa wahalifu waliokuwa wamehukumiwa kutiwa vitanzi.

Hata wakati wa mahojiano ya Jaji Mkuu, Jaji Warsame alikuwa anapasua mbirika kwa waliowania kwa sababu ya maamuzi yao kwenye kesi mbali mbali.

Wakati mmoja alimhoji vikali Jaji Jackton Ojwang wa Mahakama ya Juu hata jaji huyo akasema “nipe fursa nipumue”
Wanachama wengine wa JSC ni Jaji Mkuu (CJ) David Maraga (mwenyekiti), naibu wake DCJ Philomena Mwilu (mwakilishi wa

Mahakama ya Juu ), Mwenyekiti wa Tume ya Kuajiri Watumishi wa Umma (PSC), Katibu ni Msajili wa Idara ya Mahakama (sasa ni Ann Amadi)

Wengine ni wawakilishi wawili kutoka Chama cha wanasheria nchini (LSK) ambacho wawakilishi ni Profesa Tom Ojienda na wakili Mercy Deche. Uanachama wao utatamatika mnamo Februari 1, 2019.

 

You can share this post!

KeMU kuuza jengo lake ili kujiimarisha kifedha

Takwa la chapati kupikwa mazishini mwa mtoto aliyejinyonga...

adminleo