• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 6:55 PM
Jumapili ya Mitende ilivyoadhimishwa nchini

Jumapili ya Mitende ilivyoadhimishwa nchini

PETER MBURU na BRIAN OCHARO

Waumini wa kanisa Katoliki Jumapili walifurika kwenye barabara kote nchini wakibeba matawi ya mitende kuadhimisha siku ya ‘Jumapili ya mitende’ na mwanzo halisi wa ‘wiki takatifu’.

Mjini Nakuru, mamia ya waumini hao, wakiongozwa na askofu Maurice Muhatia wa dayosia ya Nakuru walitembea mjini humo kwa saa chache, kabla ya kufululiza hadi kwenye kanisa la Christ the King kwa ibada.

Sherehe hiyo iliandaliwa kukumbuka tukio la kishujaa yesu kristo kuingia mji wa Yerusalemu kwa unyenyekevu kabla yake kuuliwa, katika Biblia takatifu.

Matawi yaliwakilisha amani na ukaribisho mwema aliopokea Yesu alipoingia mji wa Yerusalemu na ushindi wake.

Kutembea kwa miguu nako kuliashiria unyenyekevu, hata wenye pesa na magari wakijitolea kutembea kwa mapenzi ya wokovu.

Wakati wa misa hiyo, askofu Muhatia aliwataka waumini kumwiga Yesu Kristo kwa kuwa na vitendo vya unyenyekevu, mbali na kuwasaidia wasiojiweza.

“Kwa kuwasaidia wale waliokosa katika jamii, tutakuwa tunatimiza mapenzi ya Mungu kwa kutoa kafara ya maisha ili waokoe ulimwengu,” akasema.

Mjini Mombasa, Padri Marsallius Okello wa Kanisa la Holy Ghost, aliwaomba Wakenya kuombea amani.

“Tumeanza kuona matokeo ya sala ambazo wakenya wamekuwa wakifanya  tangu Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana na tunatarajia kuwa Kenya itapata amani ambayo tumekuwa tunayotamani na kuomba,” alisema.

Padri Okello aliwaomba Wakenya kuwapa  Rais Uhuru Kenyatta na Kiongozi wa Upinzani Raila Odinga muda wa kufanya mazungumzo ili kupata suluhisho la muda mrefu ambalo litaleta utulivu wa kisiasa nchini.

Aliwahimiza  wanasiasa wote na viongozi wa kidini nchini kuhubiri amani, umoja na upatanisho ili nchi iimarishe a ki uchumi.

Kulingana na tamaduni za dhehebu la Katoliki, matawi hayo yatachomwa na jivu yake kuhifadhiwa kisha itumiwe kuighinisha siku ya jumatano ya jivu, mwaka ujao.
Waumini nao wanatarajiwa kujifungia vitu wanavyopenda kama chakula na vingine, kama mbinu ya kumtolea mungu kafara.

 

You can share this post!

Wanasiasa wataka Jubilee iwe macho Raila asije akazima...

Mkutano wapangwa kuunganisha viongozi wa Pwani

adminleo