• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Mwombeeni Mzee Moi, Gideon arai Wakenya wakumbuke babaye

Mwombeeni Mzee Moi, Gideon arai Wakenya wakumbuke babaye

Na FRANCIS MUREITHI

SENETA Gideon Moi wa Baringo amesema kuwa hali ya afya ya Rais Mstaafu Daniel Moi si nzuri, lakini anaendelea kupata nafuu.

Mzee Moi, 95, amelazwa katika Nairobi Hospital mara tatu mwaka huu. Taarifa kuhusu afya yake zimekuwa zikitolewa na msimamizi wake wa mawasiliano Bw Lee Njiru pekee.

Bw Moi alitoa kauli hiyo mnamo Ijumaa alipoongoza hafla ya kufuzu mahafali katika Chuo Kikuu cha Kabarak. Bw Moi aliwaomba Wakenya kuendelea kumwombea babake.

“Ningetaka kumshukuru kila mmoja wenu kwa niaba ya familia yangu kwa maombi yenu. Nawaomba kukubali shukrani zetu kwa kuendelea kumwombea Mzee Moi katika wakati huu ambapo hali yake ya afya si nzuri sana.

Kwa maombi, hali yake imekuwa ikiimarika kila siku,” akasema.

Kuhusu ufisadi, aliutaja kama “janga ambalo linaendelea kuwathiri vijana na ukuaji wa uchumi wa nchi.”

Aliwaomba mahafali 922 waliofuzu kwenye vitengo mbalimbali kuzingatia uwajibikaji na uzalendo na kujali maslahi ya wengine.

“Kutoka kwenu, tunatarajia kwamba mtakuwa na mienendo itakayomfaa kila mmoja katika jamii. Mnapaswa kuzingatia ukweli, hata wakati msimamo huo haumpendezi kila mtu,” akasema.

Spika wa Seneti Bw Keneth Lusaka, ambaye ndiye alikuwa mgeni mkuu mwalikwa, alisema kuwa suala kuu lililopo nchini kwa sasa ni jinsi ya kuhakikisha kuwa mfumo wa ugatuzi utamfaidi kila Mkenya.

You can share this post!

Ruto akutana na Abagusii, Abaluhya na Agikuyu kujipanga 2022

Masaibu zaidi yamwandama Gavana Waititu

adminleo