• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 1:29 PM
SHINA LA UHAI: Sababu za wewe kufanya mazoezi kupunguza uzani bila matokeo ya kuridhisha

SHINA LA UHAI: Sababu za wewe kufanya mazoezi kupunguza uzani bila matokeo ya kuridhisha

Na MARGARET MAINA

[email protected]

JE, umekuwa ukifanya mazoezi kupunguza uzani lakini hupati matokeo ya kuridhisha?

Mazoezi na lishe bora vinafaa kuambatana.

Vitu hivi viwili hutegemeana na huwezi kufikia malengo ya kuwa na afya bora bila kuzingatia mazoezi na lishe bora kwa pamoja. Hata kama unafanya mazoezi mara kwa mara, lakini lishe yako si sawia, usitegemee kupata mafanikio makubwa ya malengo yako.

Ulaji chakula kingi mara baada ya mazoezi

Kwa kawaida unapofanya mazoezi mwili hutumia nguvu nyingi. Hii ni mojawapo ya sababu zinazokufanya uhisi njaa na hamu ya kula mara baada ya kufanya mazoezi.

Jifunze au kuwa na mazoea ya kula mlo mdogo badala ya kula chakula kingi kwa sababu hurudisha mwilini nishati-lishe (calories) ulizozitumia wakati wa mazoezi, hivyo kuondoa faida ulizokuwa umezipata kwa kufanya mazoezi.

Ulaji chakula kisichofaa baada ya mazoezi

Nguvu au nishati-lishe inayokuwa imetumiwa wakati wa mazoezi hukufanya uwe na hamu ya vyakula vyenye sukari, mafuta na wanga.

Hii inatokana na mabadiliko ya vichocheo (hormones) yanayoendana na utumiaji wa nishati-lishe mwilini yanayotokea wakati wa mazoezi.

Hii ndiyo sababu ya watu wengi kuwa na hamu na vyakula vya aina hii. Lakini kumbuka kwamba kula vyakula vyenye sukari na mafuta mengi mara tu baada ya mazoezi si jambo zuri.

Epuka vitu kama soda, juisi zenye sukari nyingi na badala yake kula mlo wenye sukari ya asili kiasi kama vile juisi ya matunda isiyoongezwa sukari.

Pia kula mlo wenye kiasi kikubwa cha protini ili kuusaidia mwili kurudi katika hali yake.

Ulaji chakula kingi zaidi ya kiasi cha mazoezi unayofanya

Watu wengi hudhani kwamba, kwa kuwa wanafanya mazoezi, hawana haja ya kujali kiasi na aina ya chakula wanachokila.

Zingatia kwamba kinachotakiwa ni uwiano kati ya nishati-lishe inayoingia na ile inayotoka mwilini.

Nishati-lishe huingia mwilini kwa njia ya chakula, na hutumika au kutoka mwilini kwa kufanya mazoezi.

Kutokana na malengo mbalimbali, ni muhimu kufahamu jinsi ya kufikia uwiano utakaokufanya ufaidike.

Kwa mfano, endapo lengo lako ni kupungua uzani, ni sharti utumie nishati-lishe nyingi zaidi ya zile unazoingiza mwilini.

Maana yake ni kwamba, kiasi na kiwango cha mazoezi kizidi kiasi cha chakula unachokila.

Ukikosea uwiano huu huwezi kufaidika na mazoezi.

Kutumia kiasi kidogo cha protini na wanga kwa wingi

Mafuta hujengeka na kuongezeka mwilini kutokana na kiasi kikubwa cha nishati-lishe kinachoingia mwilini kama chakula. Vyakula vya wanga na vile vya mafuta hutoa nishati-lishe nyingi zaidi ya vyakula vya protini. Ifahamike pia kwamba uyeyushaji wa vyakula vya protini hutumia nishati-lishe nyingi hivyo kusaidia kutumia nishati-lishe ya ziada mwilini. Kwa maana hiyo, pamoja na kufanya mazoezi, vyakula vyenye protini nyingi na wanga kidogo husaidia kuzuia ongezeko la mafuta mwilini.

Pombe

Pombe ina nishati-lishe nyingi. Kwa maana hiyo unywaji pombe kupita kiwango kilichoshauriwa huchangia katika kuongeza mafuta mwilini. Hata kama unafanya mazoezi kwa kiwango kikubwa, kunywa pombe kupindukia kutarudisha juhudi zako nyuma

Kula chakula kingi chenye wanga wakati wa usiku

Wengi wetu hupumzika wakati wa usiku. Kwa maana hiyo hatuhitaji nguvu nyingi mwilini. Kula kiasi kikubwa cha wanga – vyakula vyenye kutoa nishati-lishe nyingi – hutupa nguvu ya ziada, ambayo hatuitumii. Nguvu hii ya ziada hutunzwa mwilini kama mafuta. Kwa maana hiyo, hata kama utakuwa ulichoma mafuta ya kutosha wakati wa mazoezi, ulaji wa chakula kingi cha aina ya wanga wakati wa usiku hupoteza juhudi zako za mazoezi.

You can share this post!

Dhamana ya Babu Owino yaangaziwa upya

TALAKA: Madiwani wa kike Lamu wawalaumu akina mama wapendao...

adminleo