• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Wazee wamlaani gavana kuzuia mbunge kuwapa chakula

Wazee wamlaani gavana kuzuia mbunge kuwapa chakula

Na TITUS OMINDE

WAKONGWE wanaoishi katika mitaa ya mabanda katika Kaunti ya Uasin Gishu wamemshtumu Gavana Jackson Mandago kwa madai ya kumzuia mbunge wa Kesses, Bw Swarup Mishra kuwasambazia chakula cha msaada.

Chakula hicho kililenga kusambaziwa wazee wapatao 12,000 katika Kaunti-ndogo ya Kesses.

Wazee walengwa walidai kuwa hatua hiyo ilichochechewa kisiasa, licha ya Gavana Mandago kusisitiza kwamba hatua hiyo ililenga kuwalinda dhidi ya maambukizi ya virusi vya corona.

Idadi kubwa ya wazee hao ambao wanaishi katika mtaa wa Sukunanga na Langas walisema ishara ya Dkt Mishra ilikuwa baraka iliyowasili kwa wakati muafaka. Walisema tangu kutangazwa kwa kafyu wameathiriwa vibaya na njaa.

“Dkt Mishra alikuwa malaika aliyetumwa na Mungu kutulisha na sasa amesimamishwa, serikali hii inataka tufe! Wametukataza kwenda mjini kuomba chakula na sasa wamemzuia Dk Mishra kutulisha,” alisema Bwana Steven Wanjio, mzee kutoka eneo la Sukunanga.

Kwa sasa wanataka serikali ya kaunti kushirikiana kwa haraka na Dkt Mishra na kuasambazia chakula hicho kwa kufuata hatua zote za kinga dhidi ya virusi.

Walitoa wito kwa Kamishna wa kaunti ya Uasin Gishu Abdirisack Jaldesa aingilie kati.

“Tunajua kamishna wetu si kiongozi wa kisiasa ana nia njema kwetu,tunatumai kwamba ataingilia kati na kuhakikisha tunapata chakula chetu kutoka kwa Dk Mishra,” alisema mmoja wa wazee hao.

Dkt Mishra amefichua kuwa eneo bunge lake limetenga shilingi 30 milioni kwa kununua na kusambazia wazee chakula cha msaada kwa wazee 12,000 katika wadi za Tarakwa, Kipchamo-Chereleret, Chuiyat / Tulwet na Racecourse kwa mwezi mmoja ujao.

Wakati huo huo baadhi ya wakaazi wa kaunti ndogo ya Kesses walikosoa njia ya usambazaji wa chakula hicho kutokana na hofu ya kuenea kwa Covid -19 katika mikutano iliyopangwa ili kugawa chakula hicho.

Jumapili, Kamishna wa kaunti ya Uasin Gishu alipiga marufuku usambazaji wa chakula katika eneo hilo baada ya kukutana na mbunge husika.

Kamshna huyo alisema akisema zoezi hilo linaweza kusababisha kuenea kwa virusi vya korona iwapo hatua za kiafya hazitachukuliwa.

 

You can share this post!

KAFYU: Polisi na majambazi sasa wazidisha uhalifu

CORONA: Waiguru aponea kung’atuliwa mamlakani

adminleo