• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 3:10 PM
Vyuo vya kiufundi Kiambu kuendelea kushona barakoa

Vyuo vya kiufundi Kiambu kuendelea kushona barakoa

Na LAWRENCE ONGARO

VYUO vya kiufundi katika Kaunti ya Kiambu vitaendelea kushona barakoa kwa wingi ili kutosheleza mahitaji ya wananchi.

Mnamo Jumatatu, Gavana wa Kiambu Dkr James Nyoro alizuru chuo cha Kamirithu mjini Limuru na kujionea jinsi barakoa zinavyoshonwa.

Alisema vyuo vichache vilivyoko katika kaunti hiyo vitalazimika kushona barakoa 50,000 kila wiki ili ziweze kusambazwa kwa wananchi katika kaunti hiyo.

“Ni muhimu tujitegemee kwa kushona barakoa na kusambaza kwa wananchi kwa lengo la kukabiliana na homa ya corona,” alisema Dkt Nyoro.

Alisema hatua hiyo pia itasaidia kwa njia moja au nyingine kuajiri vijana wengi.

Gavana wa Kaunti ya Kiambu Dkt James Nyoro alipozuru chuo cha kiufundi cha Kamirithu mjini Limuru Mei 11, 2020. Picha/ Lawrence Ongaro

Aliahidi kaunti hiyo itahakikisha kila mwananchi anapata barakoa kwa lengo la kujikinga na dhidi ya corona.

Alisema atawasiliana na benki kadha ili kutoka mikopo kwa wafanyabiashara wa chini kwa lengo la kuwainua kiuchumi.

Alisema ni vyema kuwainua vijana ili kupunguza shida ya ajira inayoshuhudiwa nchini kote.

Alisema kaunti ya Kiambu imeweka mikakati ili kukabiliana na coronavirus.

Tayari dawa imepulizwa katika maeneo muhimu kama maokoni, katika vituo vya magari, vituo vya polisi na makazi ya watu.

“Tunataka kuona ya kwamba tunakabiliana na janga hili ili watu waweze kurejelea shughuli zao za kawaida,” alisema Dkt Nyoro.

Baada barakoa hizo kushonwa watu watakaonufaika pakubwa ni raia kwa jumla, waendeshaji bodaboda, waendeshaji tuktuk, na wahudumu katika sekta ya matatu.

“Tunataka kuhakikisha kuwa tunapambana na janga hili tukiwa pamoja. Kila mmoja ni lazima ajihusishe kwa mtihani huo,” alisema.

Wakati wa ziara hiyo ya Limuru, gavana huyo aliandamana na naibu wake Bi Joyce Ngugi, Waziri wa Elimu katika kaunti Bi Mary Kamau, Askofu David Kariuki Ngari, kiongozi wa wengi katika bunge la kaunti ya Kiambu Bw Gedion Gachara, na diwani wa Limuru ya Kati Bw Joseph Kahenya.

Alisema ataendelea kuzuru maeneo mengine ili kujionea mwenyewe kile kinachoendelea huko.

You can share this post!

Uhuru aangusha bakora

Mkenya Wanjiru Karani ateuliwa kuhudumu katika chama cha...

adminleo