• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 9:50 AM
Wakashifu tukio ambapo baba na wanawe wawili waliuawa kwa tuhuma za kujihusisha na al-Shabaab

Wakashifu tukio ambapo baba na wanawe wawili waliuawa kwa tuhuma za kujihusisha na al-Shabaab

Na MISHI GONGO

BAADHI ya viongozi wa dini ya Kiislamu Kusini mwa Pwani wamekashifu tukio la mauaji ya baba na wanawe wawili eneo la Diani wiki iliyopita kwa tuhuma walikuwa na mafungamano na kundi la al-Shabaab.

Viongozi hao kutoka baraza la maimamu na wahubiri nchini CIPK, KEMNAC, Supkem, na Shirika la vijana wa Kiislamu KMYA na muungano wa madrasa kanda ya Kusini mwa Pwani wameyataja mauaji hayo kuwa ni ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu.

Mwenyekiti wa CIPK Kusini mwa Pwani, Sheikh Amir Zani ametaka kusimamishwa kazi kwa mkuu wa kituo cha polisi cha Diani pamoja na polisi waliohusika na mauwaji kushtakiwa.

“Serikali inapaswa kuwachukulia hatua maafisa waliotekeleza unyama huo ili kuwa funzo,” akasema.

Kwa upande wake mshirikishi wa vijana wa Supkem Kusini mwa Pwani Hamis Mwaguzo ametaja kuwa kinyume cha sheria kuwahusisha watoto na visa vya ugaidi, ikizingatiwa hawana ufahamu wowote kuhusu ugaidi.

“Watoto wasio na hatia wamepoteza maisha yao. Hawa watoto hawajui chochote kuhusu ugaidi,” akasema.

Ameitaka Mamlaka ya Kutathimini Utendakazi wa Polisi (Ipoa), kuchunguza mauaji hayo na kuwachukulia hatua maafisa waliotekeleza.

You can share this post!

Duale aponea

Mmoja wa wasichana watatu waliotekwa nyara Garissa ajinasua

adminleo