• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 9:55 AM
Wazee sita huuawa kila wiki Pwani – Serikali

Wazee sita huuawa kila wiki Pwani – Serikali

Na WACHIRA MWANGI

YAHOFIWA mkongwe mmoja huuliwa kila wiki katika kila kaunti za Pwani kwa madai ya uchawi, kwa mujibu wa Mshirikishi wa Eneo la Pwani, Bw John Elungata.

Eneo la Pwani lina kaunti sita.

Bw Elungata alisema asasi za usalama zina wasiwasi kuhusu hali hii na maafisa wanajitahidi kukabiliana na wahusika wakiwemo jamaa wa waathiriwa.

“Huwa tunapokea kisa kuhusu mzee aliyeuawa kila wiki katika kila kaunti ya Pwani. Inatia wasiwasi sana. Hata tunapolalamika kuhusu ukatili wa polisi na mizozo ya kinyumbani inayolenga wanawake, tunasahau kuna wazee wanaouliwa tu kwa sababu ya umri wao na madai ya uchawi,” akasema.

Bw Elungata alitoa changamoto kwa mashirika ya kijamii kuanzisha hamasisho kwa umma kuhusu umuhimu wa kuheshimu wazee na wakome kuwashambulia bila sababu.

Mkurugenzi Mkuu wa shirika la Haki Africa, Bw Hussein Khalid alisema uchawi hutumiwa kama kisingizio kuua wazee wakati watoto wao wanapokosa subira ya kurithi ardhi na mali nyingine.

“Tulifanya uchunguzi tukagundua vijana wanaona wazee wanaishi kwa muda mrefu kwa hivyo wanaibua madai ya uchawi ili wauawe,” akasema Bw Khalid. Alisema tatizo hilo ni sugu katika Kaunti ya Kilifi na wanashirikiana na Serikali Kuu kulitatua.

Mratibu wa Tume ya Kitaifa ya Haki za Binadamu (KNCHR) tawi la Pwani, Bi Brenda Dosio alisema inahitajika vijana watafutiwe mbinu za kupata riziki.

You can share this post!

Bingwa wa dunia mbio za mita 400 upande wa wanawake...

Morans kuanza kujifua tayari kwa Afro-Basket licha ya...

adminleo