• Nairobi
  • Last Updated March 18th, 2024 8:55 PM
Atwangwa na mkewe kama mburukenge kwa kutomnunulia nyama

Atwangwa na mkewe kama mburukenge kwa kutomnunulia nyama

Na BENSON MATHEKA

GITHUNGURI, KIAMBU

WAKAZI wa hapa, waliachwa vinywawazi baada ya jombi kupokonywa mboga na kutandikwa na mkewe kama mburukenge akimlaumu kwa kutomnunulia nyama.

Mwanadada huyo huwa anauza bidhaa sokoni kuchuma riziki.

Yasemekana kidosho huyo hakuweza kwenda kufanya kazi yake sokoni kwa sababu ya mvua mkubwa na mumewe akachukua jukumu la kununulia familia yake ilichohitaji.

Siku ya kisanga, jamaa alienda kazini ilivyokuwa desturi yake.

“Aliomba ruhusa kazini na kuondoka mapema kuliko kawaida na akiwa njiani kurudi nyumbani, aliamua kupitia katika kituo cha biashara ili ajirudishie mkono kwa kuchapa kazo nzito siku nzima,” alisema mdokezi,

Inasemekana kuwa jamaa alijitosa kilabuni na kuagiza vikombe kadhaa vya ‘Keg’ ndipo akalewa chakari.

Kulingana na mdokezi, hata baada ya kulewa, jamaa hakusahau jukumu lake la kununulia familia chakula. Alielekea dukani akanunua unga na mboga.

Inasemekana alipofika nyumbani badala ya mkewe kumpokea, alianza kumrushia cheche za matusi.

“Kitu gani mbaya na wewe? Kwa hivyo badala ya kutununulia vitu nzuri kama nyama unanunua mboga.

Kwani unafikiri sisi ni sungura wa kutafuna matawi kila siku? Mwanamume gani usiye na akili wewe. Nitakuonyesha jinsi wanaume kama wewe hufunzwa na kupata akili,” alichemka mama huyo.

Inasemekana kuwa mama watoto alimpokonya mumewe mboga na kurushia kondoo wake kabla ya kumtwanga mangumi na mateke. “Jamaa alipiga nduru zilizowavutia majirani,” alisema mdokezi.

Iliwabidi majirani hao kungilia kati na kumuokoa jamaa huku wakimlaumu mama kwa kumdharau mumewe.

Haikujulikana uhusiano wake na mkewe ulivyoendelea baada ya kisa hicho.

…WAZO BONZO…

You can share this post!

KINAYA: ‘Baba’ asisubiri hisani ya Uhuru aambiwe akalie...

JAMVI: Wito wa Atwoli watikisa msingi wa chama cha Jubilee

adminleo