• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 11:05 AM
Sijaonja pombe kwa miezi sita – Babu Owino

Sijaonja pombe kwa miezi sita – Babu Owino

Na BENSON MATHEKA

Mbunge wa Embakasi Babu Owino amedai kwamba ameacha pombe na amekuwa akiomba Mungu amsaidie kubadilisha tabia.

Kwenye video aliyopakia katika ukurasa wake wa Facebook, Bw Owino aliwataka Wakenya wamsamehe kwa vitendo na matamshi yake yaliyowaudhi.

“Nimeamua kubadilisha tabia na kuwa  kiongozi na mtu mwema,” alisema.

Alisema aliamua kuchukua hatua hiyo baada ya kutambua kwamba amewaumiza na kuwaudhi watu wengi kwa matamshi na vitendo anapowasiliana na Wakenya mtandaoni.

Alisem alianza kunywa pombe akiwa na umri wa miaka minane kwa kuwa mama yake alikuwa akiuza chang’aa kupata pesa za kuwasomesha.

“Mama yangu alinilea kwa kuuza chang’aa, hakufanya hivyo kwa sababu alipenda, alifamya hivyo kwa sababu alitaka tupate elimu, alifanya hivyo kwa sababu alitaka tupate chakula,  alifanya hivyo kwa sababu hakuwa na jingine na ilikuwa njia ya pekee ya kupata riziki,” alisema.

Alisema alionja chang’aa kwa sababy ilikuwa kawaida ya kila mtu kulewa katika mtaa wa mabanda wa Nyalenda, Kisumu ambao alilelewa.

“Tangu wakati huo nimekuwa nikinywa pombe na nimekuwa na changamoto zangu. Umefika wakati wa kubadilika na nimeamua kubadilisha mkondo wa maisha yangu, mabadiliko ambayo ninajivunia, mabadiliko ambayo familia yangu inajivunia,” alisema.

Alisema kwa miezi sita na siku tisa hajaonja pombe na huwa anaomba kila mara akiwa na mkewe. “ Ninatarajiwa kuwa mtu mwema,” alisema.

You can share this post!

Mnogeshaji video za burudani ya muziki ambaye anafanya kazi...

Uhuru apiga marufuku uuzaji pombe mikahawani

adminleo