• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 10:15 AM
Handisheki ilivyoimairsha ukuaji wa uchumi Nyanza

Handisheki ilivyoimairsha ukuaji wa uchumi Nyanza

Na RUTH MBULA

ENEO la Nyanza limefaidika na miradi ya mabilioni ya fedha kutoka kwa serikali kuu ambayo imechochea uwezo wa kiuchumi eneo hilo baada ya miaka mingi ya kutengwa na serikali za awali.

Waziri wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiang’i ambaye pia huendesha miradi ya serikali kuu, katika mahojiano na Taifa Leo alisema maeneo ya Waluo, Wakisii na Wakuria katika Kaunti ya Nyanza yamenufaika pakubwa sawa na maeneo mengine nchini.

Bw Matiang’i alisema utawala wa Rais Uhuru Kenyatta umemakinika kuhakikisha usawa nchini na azma hiyo imeangaziwa vyema katika utekelezaji wa mirdi ya maendeleo.

Waziri huyo alieleza kuwa ukuaji wa kiuchumi katika eneo hilo umechochewa na hatua ya viongozi kadhaa wakiongozwa na kiongozi wa chama cha Orange Democratic Movement Raila Odinga kuungana kisiasa.

Alisema miundomsingi ya barabara iliyoboreshwa katika maeneo ya mashinani, miundomsingi mipya ya vituo vya elimu na vilivyofanyiwa ukarabati, miradi ya kuimarisha kilimo na afya na miradi mikuu ni baadhi ya ukuaji kiuchumi uliofanikishwa na serikali kuu.

Wiki iliyopita katika mkutano ulioandaliwa katika hoteli ya Kisii State Lodge na uliohudhuriwa na Bw Odinga na mwenzake wa handisheki Rais Kenyatta, viongozi hao walikubaliana kuwa eneo la Nyanza litazungumza kwa sauti moja.

Viongozi hao waliafikiana kusonga kama kambi moja na kwamba hakutakuwepo tena migawanyiko baina ya Waluo, Wakisii na Wakuria katika Kaunti ya Nyanza.

Rais Kenyatta alipokuwa Nyanza wiki iliyopita alimwamrisha Waziri Matiang’i kuhakikisha kuanzishwa na kukamilishwa kwa miradi zaidi ikiwemo pia kukamilishwa kwa miradi iliyokwama.

Wakazi wamepongeza ukuaji kiuchumi wakisema hatimaye Nyanza inahisi uwepo wa serikali.

Katika eneo la Gusii, Kisii State Lodge, uwanja wa spoti uliofanyiwa ukarabati wa Gusii, kituo kipya cha fedha kilichofunguliwa majuzi mjini Kisii, barabara kuu yenye thamani ya Sh18 bilioni inayounganisha Ahero-Kisii-Isibania, Uwanja wa ndege wa Suneka, mradi wa maji wa Kegati na barabara yenye thamani ya Sh 3.5 bilioni inayounganisha Chebilat-Ikonge-Chabera-Kisumu, ni baadhi tu ya miradi kutoka kwa serikali kuu.

“Tuko na watu zaidi walioajiriwa katika sekta za kibinafsi na za umma,” alisema Waziri Matiang’i.

Rais alisema chini ya uongozi wa Matiang’i, taifa liko imara zaidi likiwa na visa vichache zaidi vya ukosefu wa usalama.

“Tangu nilipotoa Amri ya Rais Nambari 1 ya 2019, kazi nyingi imefanyika, mara 10 zaidi ya kile tulichokuwa tumefanya tangu nilipochaguliwa kama Rais mnamo 2013. Mbona nyinyi viongozi mruhusu watu kuja na kumtukana Bw Matiang’i?” alisema Kiongozi wa Taifa.

You can share this post!

Chama chadai BBI itahujumu mahakama

Magufuli aahidi uchaguzi huru kampeni zikitamatika leo