Amerika na Iran zaendeleza vita zikishikilia misimamo mikali
WASHINGTON, Amerika:
AMERIKA na Iran jana ziliendeleza mashambulizi ya angani huku Rais Donald Trump akitishia kuwa Iran itavamiwa zaidi iwapo haitakubali kuingia kwenye muafaka wa amani ya kudumu.
Duru zinaarifu kuwa Amerika na Iran zilikuwa zikipanga kuafikiana tena kusitisha vita lakini bado kulikuwa na masuala tata ambayo pande zote hazikuwa zimekubaliana kuzihusu.
“Amerika haitawahi kutimiza maslahi yake kwa kuvamia Iran. Vita hivi havitasaidia japo kuna hatua ambazo zimepigwa kwenye mazungumzo,” zikaarifu duru kutoka Iran.
Trump mara si moja amekuwa akisema Amerika na Iran zinakaribia kuelewana lakini hakuna ishara zozote za kuonyesha kuwa kauli yake huwa ni ya kweli.
Uhasama huo umeendelea wiki hii huku Amerika na Iran zikirushiana makombora. Ndege ya kivita ya Amerika iliangushwa na Iran karibu na Strait of Hormuz mnamo Jumatatu.
Pia Iran imekuwa ikishambulia kambi za jeshi za Amerika Mashariki ya Kati hasa Kuwait na Bahrain.
Amerika nayo imekuwa ikiendeleza mashambulizi kama mbinu ya kushinikiza Iran ifungue mkondo wa mafuta wa Strait of Hormuz.
Trump alisema kuwa Amerika inatathmini kusitisha mashambulizi iwapo tu viongozi wa Iran watakubali kuingia kwenye muafaka wa amani bila masharti makali.
Alitishia kuwa mara hii atalipua Iran iwapo nchi hiyo itaendelea kuvuta mchakato wa kusitisha vita.
Amerika na Iran zimekosa kukubaliana kuhusu Iran kustawisha viwanda vyake vya nyuklia ambavyo Amerika inasema ni hatari na si kwa ajili ya manufaa ya kawi pekee.
Iran pia inasisitiza kuwa kabla ya vita kusitishwa, Israel pia lazima ikomeshe uvamizi dhidi ya Hezbollah kule Lebanon.
Vita kati ya Amerika-Israel na Iran vilianza mnamo Februari 28 baada ya mataifa hayo mawili kuvamia Iran kwa makombora ya angani.
Maelfu ya watu wameuawa tangu wakati huo hasa Iran na Lebanon.