Habari Mseto

Magavana wakaliwa ngumu kuhusu hali ya kushtua ya hospitali za kaunti

Na SAMUEL OWINO May 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAGAVANA sasa wana hadi Juni 1, 2026 kuwasilisha mpango kamili mbele ya Seneti unaoonyesha hatua wanazochukua kukabiliana na upungufu wa wafanyakazi katika hospitali za kaunti.

Maseneta wanataka mipango hiyo ijumuishe suluhu za muda mfupi na muda mrefu, ikiwemo matumizi bora ya rasilimali zilizopo, kuboresha ustawi wa wafanyakazi na kuhakikisha hospitali zina wafanyakazi wa kutosha kwa njia endelevu.

Hatua hiyo inafuatia wasiwasi mkubwa kwamba hospitali nyingi nchini zimekosa kufikia viwango vya chini vya wafanyakazi na vifaa vinavyohitajika.

Maseneta walieleza kuwa hospitali nyingi zinakabiliwa na uhaba mkubwa wa wataalamu muhimu wa afya kama vile madaktari wa kugandisha wakati wa upasuaji, wataalamu wa picha za matibabu, madaktari wa wanawake, watoto na wapasuaji wa jumla.

Aidha, vifaa muhimu kama vitanda vya Wagonjwa Mahututi (ICU), mashine za kusafisha damu, Picha za kutumia kompyuta na vyumba vya upasuaji vinavyofanya kazi, mashine za kuhifadhi watoto wanaozaliwa kabla ya wakati pamoja na vifaa vya uchunguzi havipo au havifanyi kazi.

“Mapungufu haya yanadhoofisha moja kwa moja haki ya afya chini ya Kifungu cha 43(1) cha Katiba pamoja na azma ya serikali ya kufanikisha huduma za afya kwa wote,” alisema Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi.

Seneta Osotsi, ambaye ni mwenyekiti wa Kamati ya Uwekezaji wa Umma na Hazina Maalum za Kaunti, alikuwa akiwasilisha ripoti ya kamati hiyo kuhusu hesabu zilizokaguliwa za kampuni za maji, manispaa, hospitali na hazina mbalimbali kwa mwaka wa kifedha wa 2024/25.

Ripoti hiyo ilipitishwa na Seneti Machi 31, 2026.

Kamati hiyo pia ilibaini kuwa katika kaunti nyingi, hospitali zimehifadhi dawa zzilizopitwa na wakati bila mpango wowote wa kuziharibu.

“Hali hii inaleta hatari kubwa kwa afya ya umma na usalama wa wagonjwa kwa sababu dawa ambazo muda wake wa kutumia umepita zinaweza kutolewa kimakosa,” ripoti hiyo ilisema.

Kamati ilipendekeza hospitali ziandae mpango wa kina unaoonyesha mgao wa fedha kununua na kuweka vifaa muhimu ili hospitali za Level 4 ziweze kutoa huduma zote zinazohitajika.

Pia, magavana wametakiwa kuhakikisha kuwa wasimamizi wa hospitali wana sifa za kitaaluma zinazohitajika chini ya Sheria ya Afya na kuwasilisha ushahidi wa hatua wanazochukua ndani ya siku 60.

Miongoni mwa dosari kubwa zilizobainika ni ukosefu wa sajili kamili ya mali ya hospitali, kutopatikana kwa hati miliki za ardhi za hospitali na nyingi kutokuwa na alama rasmi za kuzitambua.

Kamati hiyo pia ilibaini kuwa baadhi ya hospitali zinafanya kazi katika ardhi ambayo haijasajiliwa rasmi kwa majina yao, hali inayoweka miundombinu ya afya katika hatari ya migogoro ya kisheria.

Kwa mfano, katika Hospitali ya kaunti ndogo ya Butere, kamati ilibaini kuwa kuna mgogoro wa mpaka wa ardhi kati ya hospitali hiyo na Shule ya Sekondari ya Butere.

Seneti sasa imewapa magavana siku 60 kuwasiliana na Wizara ya Afya ili kuharakisha kupata hati za umiliki wa ardhi na majengo ya hospitali.

Aidha, magavana wametakiwa kuhakikisha mali yote ya hospitali inatambuliwa rasmi na ripoti kuwasilishwa kwa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kuthibitisha.

“Baada ya kukamilika kuhamisha na kutathmini mali, gavana anapaswa kuandaa sajili mpya ya mali ndani ya siku 60 na kuiwasilisha kwa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali,” ripoti hiyo ilisema.