Habari

Aladwa ataka ODM iachiwe kiti cha ugavana Nairobi 2027

Na KEVIN CHERUIYOT May 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MBUNGE wa Makadara George Aladwa sasa anataka UDA iachie ODM kiti cha ugavana wa Nairobi akitaka suala hilo lijumuishwe kwenye muafaka kati ya vyama hivyo viwili kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Bw Aladwa pia ametaka ODM iruhusiwe iwasimamishe viongozi wake katika viti inavyovishikilia kwa sasa maeneo mbalimbali jijini. “Ikiwa Makadara ni ngome ya ODM, basi UDA haifai kuwa na mgombeaji hapo.
Vivyo hivyo, ODM haitakuwa na wagombeaji ambako UDA ina uungwaji mkono jijini,” akasema Bw Aladwa. Alikuwa akiongea kwenye ibada ya kanisa Jumapili ambapo alisisitiza kuwa chama hicho hakifai kusalia na makombo ilhali kinaunga mkono azma ya Rais Ruto.
“Tunataka kiongozi wa chama chetu Oburu Oginga afuatilie hili kwa sababu tumempa ruhusa ya kujadiliana na UDA. Hata hivyo, ODM lazima idumishe umaarufu wake jijini Nairobi,” akasema Bw Aladwa. Bw Aladwa mwenyewe ametangaza kuwa yuko tayari kuwania kiti cha ugavana wa Nairobi kinachoshikiliwa na Gavana Johnson Sakaja wa UDA. Bw Sakaja pia analenga kukitetea kiti chake mnamo 2027.
Kwa mujibu wa Bw Aladwa, kauli ya Katibu Mkuu wa UDA Hassan Omar kwamba chama hicho kitasimamisha wagombea kote nchini inaweza kusababisha mgongano na ODM.
“Katibu Mkuu wa UDA si mwenyekiti wa chama. Rais Ruto ndiye mtu pekee anayeweza kutoa mwelekeo wa chama, na ndiye atakayefanya mazungumzo hayo na kiongozi wa ODM,” akaongeza Bw Aladwa.
Mbunge huyo pia aliingilia mzozo kati ya Waziri wa Fedha John Mbadi na Mbunge wa EALA Winnie Odinga akisema viongozi hao wanastahili kumakinikia umaarufu wa chama badala ya malumbano yasiyokuwa na maana.
 “Wote wawili ni viongozi wetu na tunawaheshimu. Masuala yao yanaweza kutatuliwa kwa maelewano. Tumeona walichosema na hakuna kosa lolote katika hilo. Changamoto chache zinatarajiwa kujitokeza baba wa familia anapoondoka, na hilo ndilo tumekuwa tukipitia kama chama lakini polepole tunasonga mbele. Tuna imani na uongozi wa Dkt Oginga.”