Orwoba aendelea kuhemesha chama cha UDA
ALIYEKUWA Seneta Maalum, Bi Gloria Orwoba, anaonekana kulemea chama cha United Democratic Alliance (UDA) kilichompokonya wadhifa huo.
Orwoba ameshinda msururu wa kesi dhidi ya chama hicho ambacho anasisitiza angali mwanachama wake.
Wiki hii Mahakama Kuu ilikataa kusitisha utekelezaji wa uamuzi wa Mahakama ya Mizozo ya Vyama vya Kisiasa (PPDT) uliomrejesha Orwoba katika (UDA).
Hii ni baada ya mahakama kutupilia mbali maombi yaliyowasilishwa na Kamati ya Uteuzi na Kusuluhisha Migogoro ya Uchaguzi ya UDA, iliyotaka kusimamishwa kwa utekelezaji wa uamuzi wa PPDT wakati rufaa ikiendelea kusikilizwa.
Katika uamuzi wake, Jaji Linus Kassan aligundua kuwa chama hicho hakikukidhi kiwango cha kisheria kinachohitajika ili kupewa amri ya kusitisha utekelezaji wa uamuzi wakati wa rufaa, akibainisha kuwa hakikuonyesha hasara kubwa itakayopatikana endapo amri hiyo haitatolewa.
Jaji huyo alibainisha kuwa ingawa maombi hayo yaliwasilishwa bila kuchelewa, mwombaji hakueleza ni hasara gani kubwa ambayo chama kingepata iwapo utekelezaji wa uamuzi huo usingesimamishwa.
“Ni kanuni ya muda mrefu kwamba hasara kubwa ndiyo msingi wa mamlaka ya mahakama kutoa amri ya kusitisha utekelezaji,” alisema jaji huyo, akiongeza kuwa, “Iwapo mwombaji atafanikiwa katika rufaa yake, uamuzi wake utathibitishwa. Haiwezi kusemwa kwamba rufaa hiyo itakuwa haina maana.”
Mgogoro huo unatokana na uamuzi wa kamati ya nidhamu ya UDA mwezi Mei 2025 wa kumfukuza Orwoba kutokana na madai ya kukiuka kanuni za chama.
Orwoba alipinga uamuzi huo mbele ya PPDT, ambayo tarehe 20 Agosti 2025 ilitengua kufukuzwa kwake na kutangaza kuwa mchakato wa nidhamu ulifanyika kinyume cha sheria.
Katika hatua nyingine, chombo cha ndani cha utatuzi wa migogoro cha UDA kilifika Mahakama Kuu kikitaka kusitishwa kwa utekelezaji wa uamuzi huo, kikidai kuwa kinaweza kushitakiwa kwa dharau ya mahakama na kwamba uamuzi huo unadhoofisha uhuru wa ndani wa chama.
Mahakama ilitupilia mbali hoja hiyo ya dharau, ikisema kuwa maagizo ya PPDT yalielekezwa kwa chama cha UDA na si kamati yake ya nidhamu. “Swala la dharau halijitokezi,” alisema jaji.
Orwoba alikuwa amefukuzwa katika chama hicho kutokana na madai ya kutokuwa mwaminifu, madai ambayo aliyapinga akisema yalichochewa kisiasa.
Katika uamuzi wake uliotolewa Jumatano, Agosti 20, 2025, PPDT iliyoongozwa na jaji Desma Nungo ilibaini kuwa mchakato wa nidhamu wa UDA ulikiuka kanuni za haki ya asili na taratibu za haki.
“Hakukuwa na nafasi ya haki ya kusikilizwa, na mlalamikiwa hakupewa uamuzi uliopingwa,” ilisema mahakama hiyo ya mizozo.
Katika amri zake za mwisho, PPDT ilitangaza kufukuzwa kwake kuwa batili, ikabatilisha uamuzi wa kumtoa kwenye rejista ya chama, na kuzuia UDA kuchukua hatua yoyote ya kumwondoa kwa msingi wa mchakato huo uliojaa kasoro.
Baada ya kufukuzwa kwake mwezi Mei, UDA ilianza mchakato wa kujaza nafasi hiyo wazi.
Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) ilimtangaza Consolata Nabwire Wakwabubi kama mrithi wake kupitia gazeti rasmi la serikali mnamo Agosti 15.
Baadaye, Wakwabubi aliapishwa kushika wadhifa huo katika hafla iliyoongozwa na Spika wa Seneti Amason Kingi siku ya Jumatano, Agosti 20, kufuatia kutangazwa kwake kwenye gazeti rasmi la serikali.