Sonko kutabasamu mahakama ikimruhusu atoe mamilioni yaliyozuiliwa 2020
ALIYEKUWA Gavana wa Nairobi, Mike Sonko, sasa yuko huru kufikia mamilioni yake yaliyo kwenye akaunti yake ya Benki ya Equity.
Bw Sonko hangeweza kutoa pesa hizo kwa miaka sita kutokana na marufuku iliyokuwa imewekwa na mahakama kwa sababu alikuwa akituhumiwa kushiriki ulanguzi wa fedha.
Kwenye uamuzi uliotolewa Ijumaa, Jopo la Kutatua Mizozo ya Ushuru liliagiza Mamlaka ya Ukusanyanji Ushuru Nchini (KRA) iruhusu Bw Sonko atoe pesa kwenye akaunti hizo sita.
Akaunti hizo ni kati ya 10 ambazo Bw Sonko alikuwa amezuiwa kutoa pesa tangu 2020 na zilikuwa na jumla ya Sh537 milioni.
“Mahakama inaamrisha KRA iondoe notisi na barua ambazo zilizuia Bw Sonko kutoa hela zilizoka kwenye akaunti ya Equity,” ikasema uamuzi wa korti.
Fedha hizo zilikuwa zimezuiliwa mnamo Februari 2020 kwa tuhuma kuwa zilikuwa kati ya mali haramu inayodaiwa kuporwa kutoka Serikali ya Kaunti ya Nairobi.
Hata hivyo, Mahakama Kuu iliondoa amri ya kuhifadhi fedha hizo mnamo Oktoba mwaka jana na kuziachilia, kufuatia ombi lililowasilishwa na Mamlaka ya Kutwaa Mali ya Serikali (ARA).
Mahakama iliamua kuwa hakukuwa na msingi wa kisheria wa kuamuru fedha hizo kurejeshwa kwa serikali, kama ilivyokuwa ikiombwa na ARA.