Habari Mseto

Wanafunzi 25, walimu 3 wajeruhiwa katika ajali Sachangwan

Na MERCY KOSKEI August 5th, 2024 1 min read

WANAFUNZI 26, walimu watatu na mpishi mmoja wa shule ya Rockside Academy, Nairobi wanapokea matibabu katika Hospitali ya Mafunzo na Rufaa ya Nakuru na Hospitali ya Kaunti Ndogo ya Molo baada ya gari lao kuhusika katika ajali eneo la Sachangwan, Nakuru, Jumatatu, Agosti 5, 2024.
Kwa mujibu wa Kamanda ya Polisi wa Kaunti Ndogo ya Molo
Timon Odingo, basi hilo la shule lilikuwa likiwasafirisha wanafunzi kutoka Eldoret ambako walikuwa wameshiriki tamasha za muziki zinazoendelea.
Ajali hiyo ilitokea mwendo wa saa saba za mchana baada ya lori kutoka nyuma kupoteza mwelekeo na kugonga basi hilo kutoka nyuma. Baadaye lori hilo liligonga magari mengine mawili ya kibinafsi hadi yakaanguka kwenye mtaro kando ya barabara.
Watu 30 walipata majeraha katika ajali hiyo, japo waliokuwa kwenye magari ya kibinafsi hawakuathiriwa.
Maafisa wa polisi walipowasili katika eneo la ajali wenyeji na wasamaria wema walikuwa tayari wamewaondoa waathiriwa.
“Waliojeruhiwa wamekimbizwa hospitalini na sasa wanapokea matibabu. Kwa bahati nzuri hakuna aliyekufa. Maafisa wa polisi wametumwa hospitali kuendeleza uchunguzi,” Bw Odingo akasema.

Tafsiri: Charles Wasonga