• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 7:55 AM
Mfanyakazi adukua mitambo ya serikali ya Museveni na kuhepa na data ya siri

Mfanyakazi adukua mitambo ya serikali ya Museveni na kuhepa na data ya siri

DAILY MONITOR Na PETER MBURU

MADAI yameibuka kuwa mtu aliyedukua mitambo ya Wizara ya Leba nchini Uganda na kuiba taarifa za siri zenye umuhimu kuhusu uajiri ni mfanyakazi wa serikali.

Inaripotiwa kuwa wadukuzi waliiba habari na nakala za umuhimu mkuu kuhusu ajira ndani ya serikali.

Mitambo ya wizara ambayo hukagua kampuni za kutoa ajira za nje ya nchi, kuonyesha ikiwa kuna nafasi za ajira na kupigana na suala la watu kusafirishwa kwa njia haramu ilikosa kufanya kazi kwa njia ambazo hazikueleweka.

Mitambo hiyo iliwekwa baada ya malalamishi kuwa raia wa Uganda wanaofanya kazi Uarabuni wanateswa kuzidi.

Serikali iliamua kukaza kamba katika mbinu zake za kukagua habari kuhusu namna watu wanasafiri, kazi wanazoenda kufanya na ikiwa zinapatikana. Kila kampuni inayofanya biashara hiyo inapewa akaunti ambapo inasema watu inaohitaji.

Lakini wafanyakazi wa serikali wamedai kuwa ni mfanyakazi wa wizara ya Teknolojia na mawasiliano ambaye kwa ushirikiano na baadhi ya kampuni za kutafutia watu kazi walitekeleza kitendo hicho, ili kupitisha ukaguzi wa baadhi ya wafanyakazi wao.

Kamishna wa Leba katika wizara hiyo David Mugisha alisisitiza kuwa mitambo ‘ilianguka’ tu, akipinga kuwa ilidukuliwa.

“Ninawaambia kuwa mitambo ilianguka tu, sijui mlikotoa habari kuwa ilidukuliwa,” akasema Bw Mugisha.

Lakini mdokezi mmoja alieleza gazeti  la Daily Monitor kuwa wizara inamfahamu aliyedukua mitambo hiyo. Alisema, hata hivyo, wizara bado haijamchukulia hatua zozote.

Mitambo ilikuwa imeundwa kwa namna kampuni ikipokea ombi la kutafuta mfanyakazi kutoka mataifa ya nje, ingewasilisha ombi hilo kwa wizara ya Leba kabla ya kuruhusiwa.

Baada ya kuruhusiwa, kampuni inatafuta mfanyakazi na kumfanyia mahojiano, kasha anayefuzu anawasilishwa kwa wizara tena ili akaguliwe.

Majina ya wanaoruhusiwa yanawasilishwa kwa idara kadha za serikali hadi wakubaliwe kusafiri kutoka nchini.

Wadokezi walieleza kuwa tangu serikali kuanza kutumia mtindo huo, maombi mengi ya kazi yamekuwa yakikataliwa, baada ya kubainika kuwa zilikuwa feki.

Wadokezi waliendelea kuel;eza kuwa maafisa wa kampuni kwa ushirikiano na wale wa usalama na uhamiaji huwasafirisha watu kuvuka mipakani kinyume na sheria kwa kutoa hongo ya kati ya Sh300,000 na nusu milioni (za Uganda) kila mtu.

“Kampuni ambazo zinamilikiwa na wakuu wa usalama na maafisa wa serikali zinahudumiwa hata bila kulipa pesa hizo,” akasema mdokezi.

Baada ya kisa hicho cha udukuzi, serikali ya Saudi Arabia inasemekana kufahamisha wizara hiyo ya Jinsia na Leba kuwa kazi hiyo ilifanywa na watu wa ndani ya wizara yenyewe.

Wadokezi walisema kuwa maafisa wa Saudi walimtambua mdukuzi kama mfanyakazi katika wizara na kujitolea kusuluhisha tatizo hilo, lakini wizara ya Leba ikakataa msaada wake.

Mitambo hiyo ilikuwa imeundwa hibi kwamba Saudi ikiwa na nafasi za ajira ingetangaza hapo, na kampuni zikihitaji wafanyakazi pia kutangaza hapo.

Baada ya matukio hayo, kampuni ambazo zilikuwa zimehudumiwa na wateja wao kuruhusiwa kusafiri kwenda Saudi bado hazijawasafirisha.

Wadokezi walisema kuwa udukuzi ulitekelezwa kwa ushirikiano kati ya idara ya usalama na maafisa wa uhamiaji katika uwanja wa ndege wa Entebbe.

Serikali ya Saudi ilibaini kuwa kulikuwa na kisa cha aina hiyo baada ya mitambo hiyo, inayoitwa MUSANED kuruhusu watu 1660 wa Uganda kusafiri kwenda kufanya kazi, bila kukaguliwa na wizara.

Kaimu waziri wa Leba na Jinsia Peace Mutuuzo aliandikia serikali ya Saudi baada ya kubaini, akitaka maelezo kuhusu namna Waganda hao waliruhusiwa bila kupitishiwa mchakato wa kawaida.

Serikali ya Saudi, hata hivyo, ilisingizia matatizo ya kimitambo ya MUSANED kuwa sababu, ikisema kuwa timu yake ilirekebisha kosa hilo mara moja.

Wanachama wa muungano unaoshughulika na uajiri wan je ya nchi Uganda sasa wameitaka serikali kumtafuta na kumkamata mdukuzi aliyefanya hivyo.

You can share this post!

Ajabu ya mwanamume kuoa dadake atimize ndoto ya ughaibuni

Iran yamnyonga shoga mbele ya umma

adminleo