Kimataifa

Ufichuzi wa sakata ya ngono na watoto katika ‘Epstein Files’ ulivyomweka Prince Andrew pabaya

Na REUTERS, FATUMA BARIKI February 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

ANDREW Mountbatten-Windsor, kakake Mfalme Charles wa Uingereza, alikamatwa Alhamisi kwa utovu wa maadili akiwa kazini kutokana na madai kwamba alituma stakabadhi muhimu za serikali kwa Jeffrey Epstein.

Epstein ndiye mhusika mkuu wa sakata ya kushtua ya ngono na watoto na ambaye alijiua akiwa jela akitumikia kifungo cha makosa hayo nchini Amerika.

Polisi wa Uingereza kwa kawaida huwa hawataji washukiwa ila walitoa maelezo yaliyomfichua mwanamfalme huyo wa zamani, ambaye amekuwa akichunguzwa kwa madai kwamba alituma stakabadhi hizo kwa Epstein alipokuwa anafanya kazi kama balozi wa biashara.

Mwanamfalme huyo, mvulana wa pili wa marehemu Malkia Elizabeth amekuwa akikanusha kutenda maovu katika uhusiano wake na Epstein ingawa husema haonei fahari uhusiano wao.

Lakini hajakuwa akijibu maombi ya kuzungumzia sakata hiyo haswa katika siku za hivi karibuni ambapo stakabadhi nyingi zimetolewa na serikali ya Amerika zikieleza kwa kina kuhusu sakata hiyo ya watu mashuhuri duniani walivyoshiriki karamu za ngono na watoto kwa miaka mingi, almaarufu The Epstein Files.

Iwapo Andrew atapatikana na hatia anaweza kufungwa maisha gerezani na kesi yake itaendeshwa na Mahakama ya Kifalme ambayo huhusika na makosa makubwa ya jinai.

Mnamo 2022, Andrew alishtakiwa na mwanamke Mwamerika Virginia Giuffre ambaye alidai alimdhulumu kimapenzi akiwa tineja.

Hata hivyo, kukamatwa kwa Andrew kwa sasa hakuhusiani na kosa la kingono.

Mwanamfalme huyo wa zamani alilazimika kujiondoa kwenye majukumu yake ya kifalme 2019 kuhusiana na uhusiano wake na Epstein na kakake mkubwa akamvua uanamfalme kabisa mwaka jana Oktoba pale ufichuzi zaidi ulipopatikana kuhusiana na aina ya shughuli alizokuwa akijihusisha nazo na Epstein.